Boniface Mwangi ametangaza rasmi nia yake ya kuwania urais wa Kenya mwaka 2027, akielezea azma ya kuleta “mwanzo ppya” kwa taifa hilo. Mwangi alionekana kuwa sauti ya vijana dhidi ya Mswada wa Fedha wa mwaka 2024.

Mkosoaji mkuu wa serikali ya Kenya Boniface Mwangi ametangaza rasmi kwamba atawania urais katika uchaguzi wa mwaka 2027, akieleza azma ya kuleta kile alichokiita “mwanzo mpya.”

Mwanaharakati huyo mwenye umri wa miaka 42 amekuwa akiikosoa vikali serikali ya Rais William Ruto – ambaye amekabiliwa na wimbi la maandamano ya kupinga uongozi wake tangu mwaka jana.

Katika mkutano uliofanyika mjini Nairobi wakati wa maandamano ya vijana maarufu Gen Z mnamo mwaka 2024, mwanaharakati huyo alitoa mwito kwa Wakenya “kuchukua hatua sasa” na kuirudisha “Kenya mahali inapostahili kuwepo.”

Mwangi aliwahi kudai kwamba aliteswa na maafisa wa usalama nchini Tanzania alipokwenda kuonesha mshikamano na kiongozi wa upinzani nchini humo Tundu Lissu.

Alizuiliwa bila mawasiliano, akashikiliwa na maafisa wa usalama na baadaye akarudishwa Kenya huku akiwa amejeruhiwa.