Na Tatu Mohamed, JamhuriMedia, Dar es Salaam
MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amewaalika Watanzania na wakazi wa jiji hilo kujitokeza kwa wingi kushiriki kwenye hafla ya uzinduzi wa Kituo Kikubwa cha Biashara na Usafirishaji (EACLC), itakayofanyika Agosti 1, 2025 katika eneo la zamani la Stendi Kuu ya Ubungo.
Chalamila amesema uzinduzi huo utafanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye atakuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo ya kihistoria.
“Nitoe wito kwa wananchi wote, wafanyabiashara waliokwisha chukua maduka, wale wanaotarajia kuchukua, na wote wanaopenda maendeleo ya biashara nchini, wafike kushuhudia tukio hili muhimu. Ni uzinduzi wa kituo ambacho kitabadilisha taswira ya biashara si tu Tanzania, bali Afrika Mashariki kwa ujumla,” amesema Chalamila.
Chalamila ameeleza kuwa kituo hicho kikubwa kimejengwa katika eneo ambalo awali lilikuwa Stendi ya Ubungo, baada ya serikali kuhamishia shughuli hizo Mbezi. Katika eneo hilo, serikali kupitia Mamlaka ya Uwekezaji kwa kushirikiana na wawekezaji kutoka China, imefanikisha ujenzi wa kituo cha kisasa cha kibiashara.
“EACLC ni mradi wa kimkakati uliogharimu zaidi ya dola milioni 100. Kina maduka zaidi ya 2,000, maghala ya kisasa, sehemu za ofisi, maegesho ya magari, na huduma nyingi nyingine za kibiashara zinazopatikana kwa kukodishwa kwa Watanzania na hata wageni kutoka nje,” alifafanua.
Amesema Kituo hicho kilianza kujengwa Mei 2023 na sasa ujenzi wake umekamilika.
Chalamila amesema ujenzi huo ni ishara ya dhamira ya serikali kuendeleza mazingira ya biashara na uwekezaji nchini, huku akisisitiza kuwa uwekezaji huo haujachukua nafasi ya wafanyabiashara wazawa bali ni mfumo wa ubia unaowanufaisha wote.
Ametoa wito kwa wawekezaji wengine kufika kwenye Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi kupata taarifa sahihi za jinsi ya kuwekeza nchini.
