Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Njombe

MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, leo Januari 8,2026 ilitoa elimu kwa watendaji wa Serikali za Mitaa mkoani Njombe kuhusu utaratibu wa kushughulikia malalamiko na migogoro, mchakato wa kupata leseni za kuanzisha vituo vya mafuta vijijini pamoja na matumizi sahihi na salama ya gesi ya kupikia majumbani.

Akizungumza kwa niaba ya Meneja wa Kanda hiyo, Mhandisi Mwandamizi wa Maji na Usafi wa Mazingira kutoka EWURA, Bw. Dikson Semkuyu, alisema mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo viongozi hao ili waweze kuwafikishia wananchi elimu sahihi kuhusu huduma zinazodhibitiwa na EWURA.

“Tunatarajia elimu tuliyotoa itawafikia wananchi mnaowaongoza, ikiwemo mwongozo wa kutambua na kuchangamkia fursa mbalimbali za uwekezaji zinazotolewa na EWURA,” alisema Mhandisi Semkuyu.

Kwa upande wake, Katibu Kata wa Idamba, Bw. Ibrahim Ilomo, aliishukuru EWURA kwa kutoa mafunzo hayo, akisema yamewasaidia kufahamu matumizi salama ya gesi ya kupikia na kugundua kuwa zipo fursa za uwekezaji katika vituo vya mafuta vya gharama nafuu vijijini.