Na Mwandishi Wetu
Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imetoa jumla ya Hati Milki za Ardhi 1,176 wakati wa Maonesho ya Kimataifa maarufu kama Sabasaba yaliyomalizika mwishoni mwa wiki.
Katika maonesho hayo yaliyobeba kaulimbiu ya “Fahari ya Tanzania” Wizara ya Ardhi imetoa huduma mbalimbali ikiwemo hati milki za ardhi kwa wamiliki waliokamilisha taratibu za umiliki pamoja na utatuzi wa changamoto za sekta ya ardhi.
Akizungumza wakati wa hitimisho la maonesho hayo jijini Dar es Salaam, Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Dar es Salaam anayeshughulikia wilaya ya Ilala na Temeke Rehema Mwinuka alisema, kati ya hati hizo 1,176, hati 1,040 zimetolewa kwa wamiliki wa mkoa wa Dar es Salaam, 68 Pwani na 68 ni kwa mkoa wa Pwani.

Kwa mujibu wa Rehema, wizara ya Ardhi katika maonesho hayo ya Sabasaba ilihudumia zaidi ya wananchi 1,616 waliofika kuhitaji huduma za sekta ya ardhi katika maeneo mbalimbali.
“Katika maonesho ya mwaka huu wizara yetu ilijipanga kutoa huduma mbalimbali na imefanikiwa kuwahudumia zaidi ya wananchi 1,616 huku hati 1,176 zikitolewa” alisema Rehema.
Kwa upande wao, baadhi ya wananchi waliofika Banda la Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi walionesha kuridhishwa na huduma zilizokuwa zikitolewa wakati wote wa maonesho na kusisitiza umuhimu wa wizara ya Ardhi kuandaa huduma ya pamoja (One Stop Center) ili kuwarahisishia wananchi kupata huduma za sekta ya ardhi.

Walitolea mfano wa huduma ya utoaji Hati Milki za Ardhi pamoja na ukadiriaji kodi ya pango la ardhi kuwa, ni moja ya huduma iiliyopatikana kwa haraka jambo linaloonesha kuwa, wizara ilijipanga katika maonesho hayo
Jaji wa Mahakama Kuu kanda ya Arusha Mhe. Aisha Bade ambaye ni mmoja wa waliopata hati milki ya ardhi katika maonesho hayo alisema, wizara ya Ardhi kwa sasa imebadilika kwani huko nyuma kupata hati ilichukua zaidi ya mwaka.
“Niwapongeze wizara ya ardhi kwa hatua mliyofikia, huko nyuma kupata hati milki ya ardhi ni ‘issue’ lakini leo nimeipata hati yangu ndani ya muda mfupi, hongereni sana” alisema.
Naye Muigizaji wa sinema za kitanzania (Bongo Movie) Richie Mtambalike ameipongeza wizara ya ardhi kwa kutoa huduma za papo hapo hasa utoaji wa hati milki za ardhi katika maonesho ya kimataifa ya sabasaba.
“Niishukuru Wizara ya Ardhi kwa kutuletea huduma hapa katika maonesho maana kwa upande wangu nimefanikiwa kupata hati milki ya arhi hapa hapa” alisema.
Katika maonesho ya Sabasaba ya mwaka huu Wizara ya Ardhi ilitoa huduma za sekta ya ardhi kwa mkoa wa Dar es salaam ikihusisha manispaa za Kinondoni, Ubungo, Kigamboni, Ilala na Temeke, mkoa wa Pawani pamoja na Dodoma.
Vile vile, elimu kuhusiana na masula ya Sekta ya Milki, Urasimishaji Makazi Holela, Mbaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya pamoja na namna ya kujiunga na Chuo cha Ardhi Morogoro (ARIMO) katika masomo kwa ngazi ya Astashahada na Stashahada zilitolewa.