Israel imesema imefanya mashambulizi ya kulipa kisasi dhidi ya waasi wa Houthi wa nchini Yemen kwa kuyalenga maeneo kadhaa yenye mafungamano na waasi hao.

Hayo yamejiri siku moja baada ya kundi hilo kufyetua kombora la masafa lililoanguka karibu na uwanja wa ndege wa Tel Aviv.

Taarifa ya jeshi la Israel imesema mashambulizi yake ni jibu kwa hujuma zinazofanywa kila wakati na Wahouthi ikiwemo kuilenga Israel kwa makombora. Jeshi la Israel limearifu limeishambulia miundombinu muhimu ikiwemo bandari ya Hodeidah ambayo inadaiwa kwamba inatumiwa kama “lango kuu kwa waasi hao kupokea silaha hususani kutoka Iran”.

Kiwanda cha saruji cha Bajil kilichopo mashariki mwa mji wa Al-Hodeidah nacho kimelengwa. Israel inasema kiwanda hicho ni chanzo cha mapato kwav Wahouthi na saruji yake inatumika kujenga mtandao wa mahandaki ya waasi hao.