Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Kigoma

Serikali Kupitia Mradi wa kuboresha Ubora wa Elimu Sekondari (SEQUIP) imetoa kiasi cha zaidi ya Shilingi Bilioni 5.7 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya ujenzi wa shule mpya mbili za sekondari zitakazorahisisha upatikanaji wa huduma za elimu mkoani Kigoma.

Shule hizo ni pamoja na Shule ya Sekondari ya Wasichana Kigoma ambayo imejengwa katika Wilaya ya Uvinza Mkoani Kigoma huku ikiwa imeanza kutoa huduma za elimu kwa wanafunzi.

Jumla ya Shilingi Bilioni 4.1 zimetolewa na serikali kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali katika shule ya wasichana Kigoma ikiwemo maabara, vyumba vya madarasa na ofisi, Vyoo vya waliku na wanafunzi, mabweni, nyumba za walimu, Jengo la utawala, Bwalo, Jengo la TEHAMA, na Mashimo ya maji taka.

Pia serikali inaendelea na ujenzi wa shule mpya na ya kisasa ya Amali mkoani Kigoma ikiwa inajengwa katika Wilaya ya Kibondo kwa gharama ya Shilingi Bilioni 1.6

Ukamilishaji huo wa ujenzi wa Shule mpya ya Amali ambayo inajengwa ni utekelezaji wa sera mpya ya elimu ya mafunzo ya mwaka 2014 toleo la mwaka 2023.