Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Simiyu
Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kenani Kihongosi amemsifia na kumpongeza Mbunge wa Jimbo la Itilima mkoani Simiyu Njalu Silanga kwa namna anavyowasilisha bungeni hoja zenye mashiko na zenye kulenga kuwaletea maendeleo wananchi wa jimbo hilo.
Kihongosi amesema mbunge huyo ameonesha dhamira ya dhati ya kuwatumikia wananchi wake kwa kusimamia masuala muhimu ya maendeleo na kuyapeleka kwa nguvu bungeni ili kupata ufumbuzi.

Kufuatia juhudi hizo, Kihongosi amewataka wananchi wa Jimbo la Itilima kuendelea kumuamini na kumuunga mkono mbunge wao ili aweze kuendelea kupigania maendeleo yao kwa ufanisi zaidi.
Kwa upande wao, wananchi wa Jimbo la Itilima wameonesha furaha na kuridhishwa na kazi inayofanywa na mbunge wao, wakimpongeza kwa kuwaletea maendeleo mbalimbali jimboni humo ikiwemo ujenzi wa shule, vituo vya afya pamoja na kusambazwa kwa huduma ya umeme katika maeneo tofauti ya jimbo hilo.
Wananchi hao pia wamemshukuru mbunge huyo kwa kujali ustawi wa jimbo lao na kumuombea aendelee kuwa na nguvu na moyo wa kuwatumikia ili maendeleo yaendelee kuongezeka katika Jimbo la Itilima.
Yote hayo yamejiri leo Machi 8 wakati Kenani Kihongosi alipokuwa akitembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo katika Jimbo la Itilima, mkoani Simiyu, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi katika Kanda ya Ziwa.



