Na Tatu Mohamed, JamhuriMedia, Dar es Salaam
MKAZI wa Magomeni, Rahabu Mwambene, ameibuka mshindi wa gari aina ya Ford Ranger XLT katika droo ya tatu ya kampeni ya Tembocard ni Shwaa, iliyoandaliwa na Benki ya CRDB.
Droo hiyo imefanyika ikiwa ni ya mwisho katika kampeni hiyo ya miezi mitatu iliyozinduliwa rasmi Februari 14, 2025, ikiwa na lengo la kuwazawadia wateja wa benki hiyo kupitia matumizi ya kadi ya Tembocard.

Akizungumza wakati wa droo hiyo, Bonaventure Paul, Mkurugenzi wa Matawi wa Benki ya CRDB, amesema jumla ya washindi 30 wamepatikana tangu kuanza kwa kampeni hiyo.
“Baada ya kumaliza raundi ya kwanza tuliyowazawadia washindi 12 waliokwenda Mbuga ya Wanyama ya Serengeti wakiwa na wenzao, tuliendelea na droo ya pili iliyotoa washindi watano ambao wataenda Ulaya. Leo tunahitimisha kwa kumzawadia Rahabu Mwambene gari aina ya Ford Ranger,” amesema Bonaventure.
Ameongeza kuwa lengo la kampeni hiyo ni kurudisha kwa jamii na kuthibitisha nafasi ya Benki ya CRDB kama taasisi inayoongoza kwa ubunifu na huduma bora nchini.

“Benki hii imekuwa kiongozi nchini Tanzania kwa ubunifu na huduma za kisasa. Tunaendelea kuvumbua njia mpya za kuwagusa wateja wetu na kuwapa thamani zaidi ya kifedha,” aliongeza.
Kwa upande wake, Ahmed Ally, Balozi wa CRDB na Msemaji wa Klabu ya Simba, amesema kampeni hiyo imevutia wateja wengi, wakiwemo mashabiki wa Simba SC, na kutoa wito kwao kujiunga na benki hiyo.
“Mwana Simba usikae kinyonge, jiungeni na Benki ya CRDB. Pia niwatoe hofu wale ambao hawaamini kuhusu kampeni hizi, waelewe kuwa ni halali na hazina janja janja,” alisema Ahmed.
Kampeni ya Tembocard ni Shwaa ni sehemu ya mkakati wa Benki ya CRDB wa kusherehekea mafanikio na kukuza matumizi ya teknolojia ya kadi kwa njia ya kuvutia na yenye tija kwa wateja wake.


