Na Dotto Mwaibale, JamhuriMedia, Shinyanga

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mwalimu Alexius Revocatus Kagunze, ametunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) katika Ustawi wa Jamii na Uongozi wa Biashara kutoka Christian Ministerial Training University (CMTU) ya nchini Zambia.

Mbali na tuzo hiyo, pia ameteuliwa kuwa Balozi wa Amani Duniani (Peace Ambassador – AMB) na Greenling Peace Foundation kwa kutambua mchango wake katika kuhimiza amani, mshikamano na maendeleo ya kijamii.

Tuzo hizo zilitolewa Februari 27, 2026, mkoani Shinyanga katika maadhimisho ya Siku ya Amani na Upendo Duniani yaliyofanyika kitaifa, yakihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, wanaharakati wa amani na wageni kutoka ndani na nje ya nchi. Maadhimisho hayo yaliandaliwa na Umoja wa Wanamuziki Tanzania (TAMUFO).

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Khamis Said, ambaye alisema amani ni nguzo kuu ya maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kiutamaduni.

Alieleza kuwa UNESCO ilianzishwa baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia kwa lengo la kujenga utamaduni wa amani kupitia elimu, sayansi na utamaduni, ili kuzuia migogoro na kuhakikisha dunia inabaki katika mshikamano wa kudumu.

“Tunampongeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga kwa uteuzi wake wa kuwa Balozi wa Amani. Hii ni ishara kuwa viongozi wa ngazi zote wana wajibu wa kueneza ujumbe wa amani, uvumilivu na mshikamano wa kitaifa,” alisema Dkt. Said.

Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Khamis Said (kushoto) akimkabidhi cheti Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mwalimu Dkt. Alexius Revocatus Kagunze, alipotunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) katika Ustawi wa Jamii na Uongozi wa Biashara kutoka Christian Ministerial Training University (CMTU) ya nchini Zambia katika hafla iliyofanyika Februari 28, 2026 Mkoa wa Shinyanga. Kulia ni Mwenyekiti Mwanzilishi wa Greeling Global Peace Organization na mmiliki wa CMTU, Profesa Askofu Kennedy Songwe.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti Mwanzilishi wa Greeling Global Peace Organization na mmiliki wa CMTU, Profesa Askofu Kennedy Songwe, alisema wakati dunia ikiadhimisha siku ya amani, Mwalimu Kaganze ametambuliwa kwa juhudi zake za kuunganisha jamii kupitia haki na umoja.

Alisema shirika hilo linafanya kazi katika zaidi ya mataifa 30 likilenga kuinua kizazi cha viongozi wenye maono ya kuleta amani endelevu.

Naye Profesa Stephano Nzowa wa African Graduate University alisema Tanzania imejijengea sifa ya kuwa “Kisiwa cha Amani,” hivyo ni wajibu wa kila Mtanzania kuilinda na kuienzi amani hiyo kwa manufaa ya vizazi vijavyo.

Safari ya Utumishi wa Miaka 15

Mwl. Alexius Kaganze alizaliwa Machi 3, 1986, na kwa zaidi ya miaka 15 amelihudumia Taifa katika nyadhifa mbalimbali serikalini, zikiwemo:

Mwalimu

Afisa Elimu Mkuu, Ofisi ya Rais – TAMISEMI

Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga (kuanzia 2021)

Mchango Wake Katika Sekta Mbalimbali

  1. Elimu:

Amehimiza ubora wa elimu, akisisitiza walimu kuwa nguzo ya maarifa, maadili na ujenzi wa amani. Amesimamia ujenzi wa madarasa, mabweni na miundombinu ya shule za msingi na sekondari, pamoja na kuhakikisha utekelezaji sahihi wa sera ya elimu bila malipo.

  1. Ajira na Uwezeshaji Vijana:

Amekuwa mstari wa mbele kuhimiza nidhamu ya kazi, maadili na kujiajiri kwa vijana, huku akisimamia miradi ya miundombinu inayochochea uchumi wa manispaa.

  1. Biashara:

Amehamasisha utoaji wa mitaji kwa wafanyabiashara wadogo na kukutana na wadau wa sekta ya nyumba za kulala wageni ili kuboresha huduma na kukuza uchumi wa eneo hilo.

  1. Michezo:

Ameunga mkono michezo kama chachu ya kukuza vipaji, afya na nidhamu kwa vijana.

  1. Miundombinu:

Amesimamia miradi mikubwa ikiwemo ujenzi wa barabara za lami zenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 1.6, kituo kipya cha mabasi Katunda, pamoja na miradi ya elimu na afya yenye thamani ya mabilioni ya shilingi.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mwalimu Dkt. Alexius Revocatus Kagunze, akionesha cheti baada ya kutunukiwa tuzo hizo.

Katibu Mkuu wa TAMUFO, Stella Joel ndiye aliyemuibua Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga baada ya kupewa taarifa kuhusu anavyojitoa kwa jamii kuwatumikia baada ya hapo ulianza mchakato wa kujua jinsi anavyofanya kazi na hatimaye kutambulika na kutunukiwa shahada hiyo ya udaktari wa heshima.

“Tuzo ambazo amepata nataka kuwahakikishiaWanashinyanga na Watanzania kwa ujumla wao kuwa tumepata mtu ambaye atalisaidia taifa hivyo tumuombee kwani watu wa namna yake ni wachache,” alisema Joel.

Mkazi wa Shinyanga kwa zaidi ya miaka 20, Charles Luchagula, alisema mkurugenzi huyo amekuwa karibu na jamii kwa kusaidia mikopo kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu, pamoja na kuchangia maendeleo ya shule na michezo.

Kwa upande wake, Daud Moses, mmiliki wa Hope Conscious Pre and Primary School, alisema alipata msaada wa haraka katika mchakato wa usajili wa shule yake baada ya kuwasiliana na ofisi ya mkurugenzi huyo.

Akizungumza baada ya kutunukiwa tuzo hiyo, Dkt. Kagunze alishukuru CMTU kwa kutambua mchango wake akiwa hai, akisema tuzo hiyo itamhamasisha kuongeza bidii katika kuwatumikia wananchi.

“Tuzo hii inanipa nguvu mpya ya kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu na kujituma zaidi kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wa Shinyanga na Taifa kwa ujumla,” alisema.

Kwa ujumla, tuzo hiyo ni uthibitisho wa mchango wake katika kuimarisha utawala bora, kuhamasisha amani na kusimamia maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika Manispaa ya Shinyanga.

Profesa Stephano Nzowa wa African Graduate University, akimvika kofia ikiwa ni ishara ya kumtunuku Mwalimu Dkt. Alexius Revocatus Kagunze, alipotunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) katika Ustawi wa Jamii na Uongozi wa Biashara.