Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Kigoma
Asubuhi ya leo katika Ofisi za Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Ujiji, Kigoma tumemshuhudia nguli wa Utangazaji nchini, Baruan Muhuza akichukua Fomu kuwania nafasi ya kukiwakilisha Chama cha Mapinduzi katika uchaguzi Mkuu ujao kupitia jimbo la Kigoma Mjini.
Hatua hiyo inakuja mara baada ya Chama Cha Mapinduzi kutangazwa kufunguliwa kwa zoezi la uchukuaji fomu kwa wagombea wa nafasi ya ubunge, ujumbe wa Baraza la wawakilishi na udiwani.

Akiongea na Waandishi wa Habari Mkoani Kigoma mara baada ya kuchukua fomu, Baruan Muhuza amesema lengo kuu la kuchukua fomu na kuwania nafasi kupitia Chama cha Mapinduzi ni kuwakilisha Jimbo la Kigoma Mjini na kuleta mabadiliko kwa sababu mbunge aliyemaliza muda wake amefanya kazi nzuri sana, mimi sina lawama naye.
Baruan amesema kama unavyofahamu mahala popote pale kila kitu kinakwenda hatua kwa hatua, tunataka tujazie na ni wakati wa mapinduzi ya fikra ili tuweze kuleta mwamko mpya kabisa na msisimko mpya wa siasa na mwendelezo wa shughuli hasa huduma kwa wananchi kwa kupitia Ofisi ya mbunge ama mbunge mwenyewe.
“Unajua kuwatumikia Wananchi ni jambo linalotaka wito, utayari, nguvu na namna wananchi wanakupokea kwa namna gani, kwaiyo baada ya kujipima kwa miaka mitano iliyopita ambayo tulimwachia kaka yetu ambaye amemaliza muda wake, amefanya vya kutosha, nafikiri sasa tunatakiwa kujazia kutoka hapa na kwenda mbele zaidi” alisema Muhuza.
Ameongeza kuwa matarajio yake ni kuona namna ya kuibua frika mpya za kuwasaidia Vijana, kuonyesha fursa mbalimbali, na namna gani wanaweza kutumia Ziwa Tanganyika kuwanufaisha Wananchi wa Mkoa wa Kigoma.

“Lakini sio hilo peke yake ni pomoja nakuangalia fursa zilizopo kwenye kilimo, cha kisasa, (BBT) jenga kesho yako imara, wengi walifikiria ni kile kilimo kilicho baki kule Dodoma ambako yalikuwa kuwa kama majaribio au mafunzo ya wale vijana waliojitokeza wakati hule lakini sasa Rais ambaye ni mwenyekiti wa chama chetu, alihimiza kila Halmashauri hapa Nchini kuona kama inaweza kupata maeneo yakuweka maeneo hizo fursa za vijana kwenda kufanya kilimo kupitia huo mpango wa BBT” alisema Muhuza.
Aidha Baruan amesema Kigoma pia kuna maeneo ya Kilimo lakini pia Kigoma ni eneo la Wakulima na Wafanyakazi, Wafanyakazi katika maeneo mbalimbali ya huduma na shughuli kama hizo, katika eneo la kilimo amesema kunaeneo kubwa la kilimo mfano bonde la Rwiche, na maeneo mengine ambayo yanafursa nyingi ambazo bado hazijatumika kabisa sawa sawa na inavyostahili.
Amesema ukiacha huko kunashughuli mbalimbali nyingine za kijamii, ukiangalia Mji wetu wa Kigoma achilia mbali Jimbo Mkoa wote kwa ujumla wake, kwa nyakati hizi za miaka michache iliyopita Serikali Kuu na watu binafsi wameanza kuwekeza miundombinu ya shughuli mbalimbali za kimaendeleo.
“Vyuo vimejengwa hapa, Vyuo Vikuu majengo makubwa makubwa kama Hospitali ya Kanda inajengwa hapa lakini pia Viwanda cha Simenti, kiwanda cha Mabati na Kiwanda cha Magodoro na Viwanda vingine vimejengwa hapa, vingine vimekamilika na vingine vipo kwenye utaratibu wa kukamilika kwake” alisema Baruan.
Ameongeza kuwa hizi ni fursa Vijana na watu wazima waliopo katika eneo hili watavitumia vipi; utayari wa watu Kigoma hapa upo wa namna gani; kuweza kutumia hizi fursa ambazo zimeletwa na hizi shughuli.
Kwa upande mwingine Baruan amezungumzia kuhusu Ziwa Tanganyika hasa kwa upande wa huduma za Meli ya Liemba ambayo ipo kwenye ukaratabi mpya ili ije kutoa huduma bora zaidi na Meli ya Mwongozo inakarabatiwa ili ije kutoa huduma bora.
“Kuna mpango wa kujenga Meli mpya kabisa hapa Ziwa Tanganyika upande wa Kigoma ambayo ni ya Serikali, Sangala Meli inayofanya shughuli za kubeba mafuta na Meli nyingine Ndogondogo ambazo zipo hapa zote zimekarabatiwa wakati huu ili ziweze kuja kuleta ufanisi” alisema Muhuza.
Hata hivyo amewataka Wananchi walio na nguvu, Vijana waliopo katika Mkoa wa Kigoma kuiona hiyo fursa na kuona namna gani wanaweza kuitumia.
Ameongeza kuwa kumekuwa na tafiti mbalimbali, Wazee wetu wamekuwa wakivua kwa kutumia Vipe na Vimoli, ni wakati sasa wa kutafuta namna na kuita makongamano kuwashawishi Wafanyabiasha wakubwa, Wawekezaji ili waje kuwekeza katika sekta hii ya Uvuvi.
Amesema Ziwani pale kunashughuli nyingi sana za kufanya achilia mbali shughuli za usafirishaji lakini pia kwenye suala la Uvuvi, matarajio ni kuwawezesha wavuvi kufanya uvuvi wa kisasa na kuondokana na uvuvi wa kizamani ambao hausaidii sana.
“Zamani sana kulikuwa na Taasisi iliyokuwa inaitwa Yoro group, mm nikiwa kijana mdogo sana hapa Kigoma walikuwa wanavua samaki wakubwa sana, lakini sasa hivi ni ngumu sana kuwapata, japo kuwa wenzetu upande wa Congo, Zambia na Burundi wanaweza kuvua samaki wakubwa kwa sababu mifumo yao ya uvuvi” alisema
Amesema ” Kwa kiasi kuna baadhi ya watu wanavua samaki kisasa hapa kwetu bado Wavuvi wetu ni Masikini sana ukiitwa mtu mvuvi maana yake ni masikini, fukala, anavua samaki mara moja ili aweze kupeleka sokoni ajikimu kimaisha na sio kibiashara ili atajirike”.
Hata hivyo Baruan anasema anatamani kuona wanapata fikra mbadala ili waone uvuvi sio wa watu masikini, uvuvi ni wa watu matajiri sana.