Na Tatu Mohamed, JamhuriMedia, Dar es Salaam
KATIKA kuadhimisha Siku ya Utambulisho Duniani, Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) imetoa huduma maalum ya usajili kwa watu wenye mahitaji maalum katika Halmashauri ya Temeke, jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata kitambulisho cha Taifa.
Akizungumza na waandishi wa habari, Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji Vitambulisho NIDA, Edson Guyai, alisema lengo la serikali ni kuhakikisha wananchi wote, wakiwemo wenye changamoto za ulemavu na mahitaji mengine maalum, wanapata fursa ya kusajiliwa.

“Leo tumewafikia watu wenye mahitaji maalum kama sehemu ya maadhimisho haya. Ni wajibu wetu kuhakikisha kila mmoja anapata kitambulisho cha Taifa kwa kuwa shughuli zote za kijamii na kiuchumi zinahitaji utambulisho huu,” alisema Guyai.
Aidha, aliwataka wananchi kwa ujumla kuhakikisha wanajisajili mapema mara tu wanapofikisha miaka 18 ili kupunguza msongamano wa watu katika vituo vya usajili vya NIDA.
“Ukifikisha miaka 18, nenda ukajisajili mara moja. Kitambulisho hiki kinakutambulisha na kinakuwezesha kupata huduma mbalimbali muhimu za kijamii,” alisisitiza.
Kwa upande wake, Afisa Ustawi wa Jamii na Mratibu wa Watu Wenye Ulemavu wa Halmashauri ya Temeke, Restuta Bujiku, aliishukuru NIDA kwa hatua hiyo na kuwataka watu wenye mahitaji maalum kuitumia ipasavyo.

“Hii ni fursa kubwa kwetu kwa kuwa mara nyingi watu wenye mahitaji maalum hawajitokezi kwa wingi kujisajili. Tunashukuru NIDA kwa kuwaleta huduma karibu na jamii yetu,” alisema Bujiku.
Mmoja wa walemavu waliosajiliwa, Mabadi Mlawa, alisema mpango huo umewasaidia kwa kuwa wengi wao walikuwa hawana vitambulisho na kulazimika kutumia vya ndugu au jamaa.
“Nawaomba walemavu wenzangu tujitoe na tujitokeze kusajiliwa. Kupata kitambulisho chetu binafsi ni hatua kubwa kwa sababu huduma nyingi sasa zinahitaji namba ya NIDA,” alisema Mlawa.
Maadhimisho ya mwaka huu yamebeba kauli mbiu ya ‘Kitambulisho Changu, Mwamvuli Wangu’.

