Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dodoma

Taasisi ya Saratani Ocean Road, imeweka kambi katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma na kutoa huduma za kibingwa na kibobezi za uchunguzi na tiba kwa wagonjwa wa saratani.

Hatua hiyo imefikiwa ikiwa ni wiki ambayo Bajeti ya Wizara ya Afya imewasilishwa na kupitishwa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano la Tanzania.

Akizungumza na timu ya wataalamu na madaktari bingwa wa magonwja ya Saratani Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Festo Dugange, amepongeza hatua hiyo na kutoa wito kwa wabunge, watumishi wa Bunge na wageni mbalimbali wanaofika katika maeneo hayo kuitumia fursa hiyo kufanya uchunguzi wa magonjwa ya saratani.

Kwa upande wa Madaktari Bingwa wa kambi hiyo Meneja wa Huduma za Uchunguzi wa saratani na elimu kwa umma kutoka Ocean Road Dkt. Maguha Stephano, ameahidi taasisi hiyo itaendelea kuhakikisha inaendelea kutoa huduma za kibingwa na kibobezi za saratani kwa wabunge na wananchi.

Alisema, huduma mbalimbali zinatolewa ikiweno za uchunguzi, elimu , ushauri wa saratani na kuendelea kutoa huduma kupitia mkoba za kibingwa mikoani , huduma hizi maarufu kama Rais Dkt.Samia Suluhu Outreach Services zilianza kutolewa mwaka 2021, lengo likiwa ni kupunguza vifo vitokanavyo na magonjwa ya saratani nchini.

“Katika miaka hii minne ya Rais Dkt. Samia taasisi imeweza kuifikia mikoa 32 na wananchi 78,959 wamefanyiwa uchunguzi wa saratani mbalimbali,”alisema.