Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dodoma

Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan imeongeza mikopo kwa Wanafunzi wa Elimu ya juu kutoka kiasi cha shilingi bilioni 464 katika bajeti ya mwaka 2024/2025 hadi kufikia Bilioni 787 katika bajeti ya mwaka 2025/2026.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda ameyasema hayo Jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya serikali ya miaka minne katika ukumbi wa Habari Maelezo huku akisisitiza kuwa wizara yake imeongeza vituo vingine viwili vya umahiri katika elimu tiba Afrika Mashariki vinatarajiwa kujengwa Nchini ambapo itapelekea vituo hivyo kuwa vitatu.

Amesema kuwa vituo hivyo kimoja kitakuwa Benjamini Mkapa kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dodoma-UDOM na kingine kitakuwa Mloganzila hivyo kufanya kuwa na vituo vitatu vya umahiri katika elimu tiba Afrika Mashariki.

Pia Waziri Mkenda amesema kuwa kinajengwa kituo cha umahiri cha elimu tiba, Sayansi ya magonjwa ya moyo na mishipa ya damu ambapo kwa sasa zimeongeza Dola Milioni 83 na ujenzi utafanya katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete-JKCI ambapo kitakuwa ni kituo bora kwa magonjwa ya moyo na mishipa ya damu.