Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umetangaza mafanikio makubwa ya utekelezaji wa miradi ya kusambaza nishati vijijini, huku ukieleza kuwa vijiji vyote nchini tayari vimefikishiwa umeme na sasa nguvu kubwa imeelekezwa katika vitongoji.

Akizungumza katika kipindi maalum kilichorushwa na ITV Aprili 02, 2026, Mkurugenzi wa Umeme Vijijini REA, Mhandisi Jones Olotu amesema kuwa safari ya kusambaza umeme ilianza mwaka 2008 kwa bajeti ndogo lakini imezaa matokeo makubwa.

“Hadi sasa tumekamilisha Usambazaji umeme kwenye vijiji na tunaendelea na vitongoji. Tulianza na vijiji 506 na tulianza na maeneo ya kipaumbele ya Serikali ambayo yanatoa huduma ya moja kwa moja kwa wananchi ambayo ni pamoja na makao makuu ya Wilaya, shule, vituo vya afya na visima vya maji,” amesema Mha. Olotu.

Amesema miradi ya REA I, II na III imefanikisha kufikisha umeme katika vijiji vyote, huku hatua ya sasa ikilenga vitongoji 64,359 ambapo hadi sasa zaidi ya vitongoji 50,447 vimefikiwa au vina miradi inayoendelea.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Mbadala REA, Mhandisi Advera Mwijage amesema juhudi hizo zinaongezewa nguvu na miradi ya gridi ndogo zaidi ya 70 inayotumia nishati ya jua na maji.

“Kwa sasa hivi tunayo miradi mingi inayoendelea kwenye upande wa ujenzi wa gridi ndogo, tumekwishajenga zaidi ya gridi ndogo 70. Zinatumia Nishati ya maji na Nishati ya jua,” amesema.

Ameongeza kuwa miradi hiyo inasaidia kuongeza uzalishaji wa umeme na kuingiza megawati 27 katika gridi ya taifa kupitia miradi mipya inayoendelea.

Amesema kuwa REA vilevile inawezesha wananchi maeneo ya visiwani kupata Nishati ya Umeme kwa lengo la kujiletea maendeleo hasa ikizingatiwa kuwa visiwa hivyo havijafikiwa na gridi ya Taifa.

“Tunao Mradi mkubwa ambao unatekelezwa katika visiwa na kwa hatua za awali tunafunga mifumo 20,000 ya Umeme jua kwa bei ya ruzuku ili kila mwananchi aweze kunufaika kulingana na kipato chake,” amesema Mha. Advera.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano REA, Martha Chassama amesema mafanikio hayo yamechangiwa na ushirikiano kati ya REA, viongozi wa serikali za mitaa na wananchi.

Naye Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile ameipongeza REA akisema ni taasisi inayotekeleza mipango yake kwa ufanisi mkubwa ikilinganisha na nyingine za umma.