✅ Wateta kuistawisha Sekta ya Kazi, Vijana, Ajira na Huduma kwa Watu wenye Ulemavu
Na Mwandiahi Wetu, Jamhurimedia, Dar es Salaam
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Ridhiwan Kikwete amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian ambapo walizungumza masuala mbalimbali ikiwemo uhusiano uliopo kati ya Tanzania na China.

Aidha, mazungumzo hayo yamefanyika leo Mei 28, 2025 jijini Dodoma ambapo wamejadili maeneo ya kipaumbele ikiwemo Programu za uendelezaji Ujuzi kwa nguvu kazi, kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi na sekta isiyo rasmi ili kuongeza fursa za ajira pamoja na kukuza ushirikishwaji wa Watu wenye Ulemavu kwenye shughuli za kiuchumi.
Vile vile, wamejadili suala la kubadilishana uzoefu kwa kuwajengea uwezo vijana pamoja na wafanyakazi kuhusu ukuaji wa teknolojia katika nyanja mbalimbali.
Kwa upande wake, Balozi wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian
ameishukuru serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuimarisha ushirikiano baina ya nchi hizo mbili.
“Serikali ya China itaendelea kuwajengea uwezo wa kitaalamu Vijana wa Tanzania kwa kutoa mafunzo yatakayo wawezesha kupata ujuzi utakaowawezesha kumudu shindani katika soko la ajira ndani na nje ya nchi” amesema.
