Na Joseph Mahumi, WF, Dar es Salaam
Serikali ya Tanzania imewakaribisha wawekezaji kutoka Uturuki kuwekeza katika sekta za kimkakati zikiwemo miundombinu, nishati na kilimo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuharakisha maendeleo ya uchumi na kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.
Wito huo umetolewa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati alipokutana na Balozi wa Uturuki nchini, Mhe. Dkt. Bekir Gezer, akiambatana na ujumbe kutoka Benki ya EXIM ya Uturuki, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam.
Alitoa wito wa Uturuki kushiriki katika ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji hususan katika ujenzi wa vipande vya Lot 3 na Lot 4 vya Reli ya Kisasa (Standard Gauge Railway (SGR)), ambavyo Benki ya EXIM ya Uturuki imeonesha nia ya kufadhili, ikiwa ni vipande muhimu katika kuunganisha mtandao wa reli unaoendelea kujengwa kutoka Dar es Salaam kuelekea maeneo ya ndani ya nchi na nchi jirani, vitakavyo chochea biashara ya kikanda na kimataifa.
“Kukamilika kwa mradi huu wa SGR, kutaiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha usafirishaji na biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, na utafungua fursa za uwekezaji katika maeneo yanayozunguka reli hiyo na kuunda korido ya maendeleo ya kiuchumi” alisema Mhe. Balozi Omar
Aliongeza kuwa Katika sekta ya nishati, Tanzania imepiga hatua kubwa kwa kuongeza uzalishaji wa umeme kutoka megawati 1,700 hadi zaidi ya megawati 4,000 ndani ya kipindi cha miaka michache iliyopita, kufuatia kukamilika kwa mradi wa Julius Nyerere Hydropower Project na Serikali inalenga kuongeza uzalishaji huo hadi kufikia megawati 8,000 ifikapo mwaka 2030, na hatimaye megawati 15,000 na kutoa wito wa uwekezaji zaidi kutoka Uturuki ikiwemo Exim Bank kupitia mfumo wa ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP).
Kwa upande wa kilimo, Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa Tanzania ina fursa kubwa kutokana na rasilimali zake za ardhi yenye rutuba na vyanzo vya maji, na inaweza kujifunza kupitia uzoefu wa Uturuki katika kubadilisha sekta hiyo kutoka uzalishaji wa kawaida hadi wa kisasa unaotumia teknolojia za kisasa na kuisaidia Tanzania kufikia lengo la kuwa ghala la chakula barani Afrika.
Kwa Upande wake Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Mhe. Dkt. Bekir Gezer, alisema kuwa Tanzania na Uturuki ni nchi ndugu zenye uhusiano wa muda mrefu uliojengwa juu ya misingi ya kuaminiana, urafiki, mshikamano na kuheshimiana.
Mhe. Dkt. Gezer, alisema kuwa Tanzania ina umuhimu mkubwa kutokana na utulivu wake wa kisiasa na kiuchumi pamoja na wingi wa rasilimali za asili, na eneo la kijiografia la linaifanya kuwa kitovu muhimu cha biashara na usafirishaji, hali inayovutia si tu Uturuki bali pia mataifa mengine duniani kiuwekezaji.
Aliongeza kuwa kupitia taasisi kama Benki ya EXIM ya Uturuki na kampuni zake, nchi hiyo iko tayari kuendelea kushirikiana na Tanzania katika miradi ya maendeleo kwa manufaa ya pamoja.
Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Kamishna wa Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justine, Kamishna Msaidizi wa Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bi. Tiba Kisonga, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Ellen Mahudu, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Standard Chartered, Bw. Herman Kasekende, Mkurugenzi wa Fedha za Miradi na Uhusiano ya Kimataifa wa Benki ya EXIM ya Uturuki, Bi. Hatice Ürkmez, na maafisa wengine waandamizi wa Wizara ya Fedha na Benki ya EXIM ya Uturuki.




