Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Serikali imetoa wito kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwekeza kwenye ujenzi wa viwanda vya kutengeneza vifaa tiba na dawa kwa ajili ya matibabu ya maradhi ya afya ya kinywa na meno, ili kuimarisha huduma za afya na kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma za Afya ya Kinywa kutoka Wizara ya Afya, Dkt. Baraka Nzobo, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba, wakati wa kufunga maonesho ya siku mbili ya bidhaa na huduma za afya ya kinywa na meno (Tanzania Dental Expo), yaliyofanyika Mei 30 na 31, jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi msaidizi wa huduma za tiba na meno katika wizara ya Afya ambaye pia ni Mwenyekiti wa bodi ya maonesho ya Tanzania Dental Expo, Dkt. Baraka Nzobo (kulia) aliyemuwakilisha Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na wajumbe wa bodi hiyo punde mara baada ya kufungwa kwa maonesho hayo yaliyofanyika kwa siku mbili katika kumbi zilizopo Mlimani City jijini Dar es Salaam, (wapili kulia) ni Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Dental Expo, Dkt. Ambege Mwakatobe, (kushoto) ni Mjumbe wa bodi hiyo, Dkt. Leonora Assevi na (wapili kushoto) ni Rais wa ‘Tanzania Dental Association’, Dkt. Gemma Berege.

“Kwa kupitia maonesho haya, napenda kuwakaribisha wawekezaji wa huduma za afya ya kinywa na meno kuchangamkia fursa zilizopo hapa nchini kwa kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya kuzalisha bidhaa na vifaa tiba vya afya ya kinywa na meno,” alisema Dkt. Nzobo.

Dkt. Nzobo alibainisha kuwa jiografia ya Tanzania inaiweka nchi katika nafasi ya kipekee ya kibiashara, kwani viwanda vitakavyoanzishwa vitahudumia si tu soko la ndani bali pia nchi jirani, hivyo kuongeza pato la taifa na kutoa ajira kwa Watanzania.

“Serikali ipo tayari kushirikiana na wadau wote wa sekta ya afya ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora. Ushiriki wetu katika maonesho haya ni ushahidi wa dhamira hiyo,” aliongeza Dkt. Nzobo.

Mkurugenzi wa Tanzania Dental Expo Dkt. Ambege Jack Mwakatobe ambaye pia ni muwakilishi chama cha wataalam wa afya ya kinywa na meno katika Chama cha Ushirika wa Kinywa na Meno duniani (FDI) akizungumza Rais wa Shirika la Meno na Makamu wa Rais wa shirikisho la taaluma ya matibabu nchini Misri, Dkt. Ehab Heikal (kulia) wakati wa maonesho yaTanzania Dental Expo yaliyofanyika mwishoni wa wiki katika kumbi zilizopo Mlimani City jijini Dar es Salaam.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Tanzania Dental Expo, Dkt. Ambege Mwakatobe, alisema lengo la kuandaa maonesho hayo limefanikiwa kwa kiwango kikubwa kwa kuwa yamewakutanisha wataalamu kutoka ndani na nje ya nchi pamoja na watoa huduma, watengenezaji wa vifaa tiba na wananchi kwa ujumla.

“Maonesho haya yamekuwa chachu ya maendeleo kwa wanataaluma wa afya ya kinywa na meno. Wamejifunza, wamebadilishana uzoefu na kuona teknolojia mpya zitakazowasaidia kuboresha huduma wanazotoa,” alisema Dkt. Mwakatobe.

Aidha, aliwahimiza wananchi kujenga utamaduni wa kuchunguza afya ya kinywa na meno mara kwa mara ili kuweza kugundua mapema matatizo yoyote yanayoweza kujitokeza.

Dkt. Mwakatobe pia alieleza kuwa, licha ya kuwa ni mara ya kwanza kwa Tanzania kuandaa maonesho kama hayo, wataalamu wengi wameonyesha furaha na hamasa ya kushiriki tena katika miaka ijayo kutokana na manufaa waliyoyapata.

Dkt. Aloyce John kutoka Mwanza, mmoja wa washiriki wa maonesho, alisema maonesho hayo yamewapa motisha kubwa ya kuendelea kujifunza, hasa kutokana na uwepo wa vifaa vya kisasa vinavyohitaji ujuzi wa ziada ili kuvitumia kwa ufanisi.

“Matatizo ya afya ya kinywa na meno yanaongezeka kwa kasi nchini kutokana na ukosefu wa elimu sahihi juu ya usafi wa kinywa na ulaji wa vyakula vinavyoharibu meno. Tunahitaji kuongeza juhudi katika kutoa elimu hiyo,” alisema Dkt. Aloyce.

Naye mwanafunzi wa fani ya afya ya kinywa kutoka Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS), Bw. Boaz Nkono, alisema maonesho hayo yamewapa picha halisi ya changamoto na fursa zilizopo katika sekta hiyo.

“Awali nilidhani fursa ni kuajiriwa tu, lakini kupitia maonesho haya nimegundua kuwa ninaweza kujiajiri na hata kuwaajiri wengine. Hii ni fursa ya kipekee kwa sisi vijana,” alisema Bw. Nkono.

Wadau mbalimbali wa afya ya kinywa na meno wakifuatilia mawasilisho mbalimbali kutoka kwa madaktari wabobedhi katika fani hiyo, ( hawapo pichani) kabla ya kufungwa kwa maonesho hayo ya Tanzania Dendat Expo yaliyofanyika kwa siku mbili katika kumbi zilizopo Mlimani City jijini Dar es Salaam,