Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam
Serikali imewaelekeza wakurugenzi wa halmashauri zote nchini kuhakikishia taasisi zao zikiwemo za elimu zinahamia katika nishati safi ya kupikia na kuachana na kuni na mkaa ifikapo Juni 30, 2026, hatua itakayosaidia kupunguza ukataji wa miti kwa ajili ya niashati hiyo isiyo safi.
Maelekezo hayo yametolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Festo Dugange alipofanya ziara katika Shule ya Sekondari ya wasichana Mabwe Tumaini iliyopo Manispaa ya Kinondoni mkoani Dar es Salaam .
Ziara hiyo ni kwa ajili kukagua utekelezaji wa maelekezo ya Serikali kwa taasisi zinazolisha watu zaidi ya 100 kutumia nishati safi ya kupikia na kuhamasisha matumizi ya nishati hiyo.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Dkt. Dugange alisema dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kuwa Tanzania inasimamia utunzaji wa mazingira kwa kuendelea kupanda miti katika maeneo mbalimbali nchini.
Alisema tayari imeandaa mpango wa kukijanisha Tanzania ambao unalenga kupanda miti kila sehemu kwenye taasisi mbalimbali huku akionesha kuridhishwa na hali ya upandaji miti katika shule hiyo.
Alipongeza Manispaa ya Kinondoni kwa utunzaji wa mazingira sanjari na kutekeleza maelekezo ya Serikali kwa kuanza matumizi ya nishati safi ya kupikia katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Dkt. Dugange alisema ukataji wa miti unachangia kwa kiasi kikubwa mabadiliko ya tabiachi kwani mvua zitakosekana na pia kwenye maeneo yasiyo namiti hutokea mafuriko na kuathiri makazi na mashamba ya wananchi.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni Bi. Hanifa Hamza alisema manispaa hiyo imejipanga kuhakikisha shule zote za sekondari na msingi zinatekeleza agizo la Serikali kutumia nishati safi ifikapo Juni 30, 2026.
Alisema kuwa katika kufanukisha hilo wataendelea kutoa elimu kwa wakuu wa shule na kusimamia utekelezaji wa maelekezo hayo na kuhakikisha shule zote zilizobaki zinahama kutoka nishati chafu na kuanza kutumia nishati safi.
Awali akitoa taarifa fupi kuhusu matumizi ya nishati safi, Mkuu wa shule hiyo, Bi. Selemia Miyangaa alisema awali walikuwa wakitumia kuni kwa ajili ya kupikia ambayo ilikuwa ni shilingi milioni 3 kwa mwezi.
Alisema kuwa kutokana na changamoto hiyo, mwaka 2019 shule ilianza kutumia gesi kupikia ambayo ni shilingi milioni 2 kwa miezi ambayo ni gharaamu nafuu ukilinganisha na nishati chafu ya awali.
Bi. Miyanga aliongeza kuwa matumizi ya nishati ya gesi yana faida kubwa kwani licha ya kuivisha chakukula vizuri pia wanalinda mazingira kwa kuepuka kukata miti kwa ajili ya kuni.
Itakumbukwa kuwa tayari Serikali imezindua Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati safi ya kupikia (2024-2034) ambao unatoa mwelekeo wa nchi kuhamia katika nishati safi.
Halikadhalika, mkakati huo unalenga kuhakikisha kuwa asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ikiwemo gesi, umeme na zinginezo ifikapo mwaka 2034.







