Na Tatu Mohamed, JamhuriMedia, Dar es Salaam

KATIBU wa Jumuiya na Taasisi za Kiislam Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda, amejiunga rasmi na Chama cha ACT Wazalendo ambapo amesema hatua yake ya kujiunga na chama cha siasa inalenga kupata jukwaa la kuwaelimisha wananchi kuhusu ajenda kuu ya taifa ya Katiba Mpya.

Hafla ya mapokezi yake imefanyika leo, Juni 5, 2025, katika makao makuu ya chama hicho Magomeni, Dar es Salaam, ikiongozwa na Kiongozi wa Chama Dorothy Semu na viongozi wengine waandamizi.

Akizungumza baada ya kukabidhiwa kadi ya uanachama na Katiba ya chama, Sheikh Ponda amesema ameamua kuchangia nguvu katika Operesheni Linda Demokrasia, inayolenga kurejesha haki, uwazi, na usawa kwenye mchakato wa uchaguzi nchini.

Amesisitiza kuwa mapambano ya kudai haki si ya mtu mmoja wala chama kimoja, bali yanahitaji mshikamano wa kila Mtanzania.

“Amani ya kweli haiwezi kupatikana wakati ambapo kura zinaibiwa, wananchi wananyamazishwa, na sheria zinageuzwa silaha dhidi ya wapigania haki,” amesema Sheikh Ponda.

Amesema kuwa ushiriki wa viongozi wa dini kwenye siasa ni muhimu kwa ajili ya kulinda maadili ya taifa na kuleta mabadiliko ya kweli.

Aidha, ametaja matukio kadhaa ya ukiukwaji wa haki, ikiwemo kuvamiwa kwa nyumba za ibada, watu kutekwa na kuteswa na ‘wasiojulikana’, pamoja na kuzuiwa kwa wananchi kufuatilia kesi za viongozi wao.

“Sheria inapaswa kulinda wananchi, si kuwatesa, na kwamba mfumo wa sasa wa nchi umepotoka na kuathiri maisha ya watu wengi. Kwahiyo lengo Kuu la kujiunga na ACT Wazalendo ni kusimamia utawala wa sheria na kudai uchaguzi huru na wa haki,” amesema Sheikh Ponda.

Ametoa wito kwa Watanzania wote, hususan vijana, wanawake, wazee, na viongozi wa dini kushiriki kikamilifu katika mapambano ya kudai haki za msingi.

Awali akimkaribisha Sheikh Ponda, Kiongozi wa Chama hicho, Dorothy Semu amesema ACT Wazalendo imepata heshima kubwa kutokana na kujiunga kwake.

“Tunashukuru kwa heshima kubwa aliyotupatia kwa kujiunga na Chama chetu, kwani ninaimani kujiunga kwako kutasaidia kuongeza nguvu kwenye Kampeni yetu ya kupigania haki na kulinda Demokrasia,” amesema Semu.

Akizungumzia Sheikh Ponda, Wakili Peter Madeleka amesema ni mpiganaji, mpambanaji, mzalendo na muadilifu.

“Kwetu sisi kupokea mpambanaji ni heshima ya kipekee, kuna majukwaa mengi ambayo angechagua kwenda lakini akaiona ACT Wazalendo itamfaa kuendeleza yale yote ambayo ameyaona.

“Hujafanya makosa kwani mimi mpiganaji mwenzako niko hapa, tutakutana na kila aina ya ushirikiano na Upendo wa kutosha,” amesema Madeleka.