Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) zimeendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuhakikisha zinaongeza wigo wa fedha za mazingira kupitia vyanzo vya mapato vya ndani na nje ili kusaidia juhudi za Zanzibar kukabiliana na athari hizo.
Aliongeza kuwa Mkakati uliopo sasa ni wa kuongeza wigo wa upatikanaji wa fedha za mazingira kuhakikisha yanahifadhiwa na kuwa katika Dira ya 2025 na kwa umuhimu wa pekee sekta hiyo imepewa nguzo yake ya utekelezaji.
Alisema hayo wakati akijibu akijibu swali la msingi la Mbunge wa Shaurimoyo, Mhe. Mattar Ali Salumu aliyeuliza Serikali haioni haja ya kuongeza wigo wa fedha za mazingira ili kusaidia juhudi za Zanzibar kukabiliana na athari hizo.
Akiendelea kujibu swali hilo, Dkt. Dugange alieleza kuwa hatua zilizochukuliwa ni pamoja na kutenga fedha kupitia Bajeti ya SMZ, kutafuta fedha kutoka katika Mifuko mbalimbali ya kimataifa ya Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi.
Alitaja Mifuko hiyo kuwa ambayo ni pamoja na Mfuko wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (Adaptation Fund, AF), Mfuko wa Mazingira wa Dunia (Global Environment Facility, GEF) na Mfuko wa Mabadiliko ya Tabianchi (Green Climate Fund, GCF) na kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa Maendeleo ili kuongeza wigo wa fedha kupitia misaada na mikopo nafuu.


