OR-TAMISEMI, Kenya

Tanzania imeendelea kung’ara katika mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Shule za Msingi na Sekondari Afrika Mashariki (FEASSA 2025) baada ya kufanya vizuri kwenye michezo ya riadha na kujinyakulia medali nyingi katika fainali zilizofanyika mjini Kakamega, Kenya.

Mashindano hayo ya riadha yalihusisha mbio fupi, mbio za kati na mbio ndefu, ambapo vijana wa Tanzania walionesha kasi, ustahimilivu na maarifa makubwa yaliyowawezesha kushinda nafasi za juu.

Katika michezo ya miruko ikiwemo kuruka chini, kuruka juu na miruko mitatu, wanariadha wa Tanzania waliendelea kutamba kwa kutwaa medali na kuonyesha uwezo mkubwa dhidi ya wapinzani wao. Aidha, kwenye michezo ya mitupo kama vile tufe, mkuki na kisahani, Tanzania iliibuka na ushindi uliodhihirisha maandalizi na vipaji vikubwa walivyonavyo wanamichezo wake.

Mafanikio haya yamewaweka wanariadha wa Tanzania kwenye nafasi ya heshima katika mashindano ya FEASSA 2025, huku wakipongezwa kwa nidhamu, ujasiri na kujituma vilivyowapa nafasi ya kupanda majukwaa ya medali mara kwa mara. Bila shaka, matokeo haya yamezidi kuongeza ari na matumaini ya kuendeleza michezo ya Tanzania kimataifa.