Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam

TUME ya TEHAMA (ICTC) imeshiriki kikamilifu katika sherehe za Siku ya Wafanyakazi Duniani mwaka huu ambazo kwa Jiji la Dar es Salaam, ziliongozwa na Mkuu wa Mkoa huo, Albert Chalamila.

Ikiwa ni taasisi ya umma inayosimamia utelezaji wa Sera ya Taifa ya TEHAMA na kuikuza sekta husika nchini, Tume ya TEHAMA iliungana na taasisi nyingine kuadhimisha siku hii muhimu kwa watumishi wa umma na sekta binafsi.

Watumishi wa Tume hiyo walijumuika katika maandamano yaliyofanyika kwenye Viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe katika Manispaa ya Kinondoni, wakiwa wamevalia mavazi rasmi yenye nembo ya Tume, wakionesha mshikamano, nidhamu na uzalendo.

Akizungumza baada ya sherehe hizo, Mkuu wa Kitengo cha Utawala na Rasilimali-Watu wa Tume ya TEHAMA, Bi. Flora Salakana, alisema ushiriki wa Tume katika maadhimisho hayo ni ishara ya kuthamini mchango wa rasilimali watu katika kukuza sekta ya TEHAMA na maendeleo ya taifa kwa ujumla.

“Watumishi wetu ndio nguzo kuu ya utekelezaji wa majukumu ya Tume. Tunathamini sana kazi yao na tunaendelea kuboresha mazingira ya kazi ili kuongeza ufanisi,” alisema Bi. Salakana.

Kaulimbiu ya mwaka huu, “Uchaguzi Mkuu 2025 utuletee Viongozi wanaojali Haki na Maslahi ya Wafanyakazi,” imeakisi dhamira ya kutaka kuimarishwa kwa ustawi wa wafanyakazi unaimarishwa, ikiwemo kwenye sekta ya TEHAMA ambayo ni kiini cha uchumi wa kidijitali.

Tume ya TEHAMA itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha TEHAMA inatumika kuboresha huduma za umma, kuongeza fursa za ajira na kuinua uchumi wa taifa kupitia ubunifu na matumizi sahihi ya teknolojia.