Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mheshimiwa Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb) amewasilisha taarifa ya ufafanuzi kwa Kamati ya Mawaziri wa Jumuiya ya Madola Wanaosimamia Utekelezaji wa Tunu za Jumuiya hiyo (Commonwealth Ministerial Action Group-CMAG) kufuatia vurugu zilizotokea nchini tarehe 29 Okotba 2025, katika kikao chake cha dharura kilichofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 05 Desemba 2025.
Akiwasilisha taarifa hiyo, Mhe. Kombo amesema matukio yaliyotokea tarehe 29 Oktoba 2025, ambayo hayakutarajiwa kutokea yalisababisha uharibifu mkubwa, ukiwemo wa miundombinu, ofisi za Serikali, mali za raia, kuchomwa moto kwa vituo vya polisi na kusababisha vifo na majeruhi.
Amesema kufuatia vurugu hizo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan aliunda Tume Huru ya Uchunguzi wa Vurugu zilizotokea wakati na baada ya uchaguzi. Tume hiyo imepewa miezi mitatu kukamilisha jukumu hilo na kuwasilisha taarifa kamili kwa Mhe. Rais.
Tume hiyo imelenga kuchunguza na kubaini chanzo cha matukio hayo na kutoa mapendekezo ya nini kifanyike, hatua ambayo itakuwa ndiyo msingi wa majadiliano na hatua mbalimbali zitakazosaidia kuleta maridhiano na maelewano nchini.
Mhe. Kombo pia aliieleza Kamati ya CMAG dhamira ya Tanzania ya kuendelea kushirikiana na Jumuiya ya Kimataifa ili kuimarisha amani na maendeleo, na aliiomba kamati hiyo kuivumilia Tanzania katika kipindi hiki ambacho Tume ya Uchunguzi inatekeleza jukumu hilo, itakapokamilisha na kuwasilisha ripoti yake, Tanzania itafungua milango ya majadiliano na Jumuiya ya Kimataifa.
.



