Waziri wa Kazi wa Cuba Marta Elena Feitó Cabrera amelazimika kujiuzulu baada ya kutoa maoni ya kukanusha kuwepo kwa ombaomba katika kisiwa hicho kinachoongozwa na Wakomunisti.

Waziri alikuwa amesema hakuna kitu kama “ombaomba” nchini Cuba na watu wanaopitia takataka walikuwa, kimsingi, wakifanya hivyo kwa hiari ya kupata “fedha rahisi”, kama alivyoelezea.

Maoni yake, yaliyotolewa katika kikao cha bunge, yalikasolewa pakubwa na Wacuba ndani na nje ya nchi, na kulaumiwa na rais wa kisiwa hicho, Miguel Díaz-Canel.Alilazimika kujiuzulu hivi karibuni.

Viwango vya umaskini na uhaba wa chakula vimezidi kuwa vibaya nchini Cuba huku ikiendelea kukabiliwa na mzozo mkubwa wa kiuchumi.

Feitó Cabrera alitoa maoni hayo mapema wiki hii katika kikao cha Bunge la Kitaifa.

“Hakuna ombaomba nchini Cuba. Kuna watu wanajifanya ombaomba ili kupata pesa kirahisi,” alisema.

Katika kujibu madai yake kwamba hakukuwa na ombaomba nchini Cuba, lakini watu waliojigeuza kuwa ombaomba, mwanauchumi wa Cuba Pedro Monreal aliandika kwenye X: “Lazima kuna watu pia waliojificha kama ‘mawaziri'”.

Waziri huyo hakuelewa ghadhabu ambayo maoni yake yangesababisha na ni kwa kiwango gani yalionyesha uongozi wa nchi kama usio na hisia, ubabe na uliotengwa kabisa na mapambano mabaya ya kiuchumi ya Wacuba wa kawaida.

Idadi ya wanaharakati na wasomi wa Cuba walichapisha barua ya kutaka aondolewe, wakisema maoni hayo ni “tusi kwa watu wa Cuba”.