AFYA: Usizidharau dalili hizi

Hizi ni dalili mbalimbali zinazojitokeza kwenye miili yetu. Japo zinaweza zisiashirie tatizo, lakini kama ikitokea zinajirudia mara kwa mara ni vyema kupata vipimo na ushauri wa kiafya.

Dalili ya kwanza ni udhaifu wa kwenye miguu na mikono kunakoambatana na ganzi.

Ikiwa sehemu za mikono na miguu zinadhoofika, zinakosa nguvu na kupata ganzi na hasa dalili hizi zikitokea hadi usoni, inaweza kuwa ni dalili ya kiharusi na hasa kama hali hii inatokea upande mmoja tu wa mwili.

Sambamba na dalili hizi, kiharusi pia huambatana na dalili kama vile unakosa `balansi’ wakati wa kutembea, unapata kizungunzungu na kushindwa kutembea vizuri.

Nikukumbushe tu msomaji, kiharusi ni ugonjwa unaosababishwa na matatizo ya usambazwaji wa damu kwenye ubongo  kutokana na kuziba au kupasuka kwa mirija inayosambaza damu kwenye ubongo na kusababisha chembechembe za damu kufa.

Kiharusi kwa kitaalamu kinaitwa stroke na ni maarufu kwa jina hili. Kiharusi ni moja ya magonjwa yanayoongoza kusababisha vifo vya ghafla kwa miaka ya hivi karibuni.

Hivyo pata msaada wa kitabibu haraka ikitokea unapatwa na dalili hizi pamoja na dalili zingine kama kutoona vizuri, maumivu makali ya kichwa, kuhisi kuchanganyikiwa au kupata shida katika kuongea.

Dalili nyingine ni maumivu ya kifua. Maumivu ya kifua na hasa yanayoambatana na joto kali na kutokwa na jasho, upumuaji wa shida na hata kichefuchefu, yanapaswa kutafutiwa ufumbuzi wa kitabibu haraka.

Maumivu ya kifua yanayodumu kwa muda mrefu yanaweza kuwa ni ishara ya magonjwa ya moyo au shambulio la moyo na hasa kama yakitokea wakati wa kufanya mazoezi au hata shughuli yeyote inayofanya mwili utumike.

Lakini pia maumivu ya mara kwa mara ya kifua yanaweza kuashiria tatizo lingine tofauti na moyo,kama vile kuganda kwa damu kwenye mapafu  au mzunguko wa damu kutokuwa sawa kwenye mapafu.

Pamoja na hayo, ni vyema kumuona daktari haraka endapo kifua kinabana na hali hii ikiwa ni ya kujirudia rudia.

Lakini dalili nyingine ni mkojo unaoambatana na damu. Yapo matatizo mengi ambayo yamezoeleka yanayoweza kusababisha kutoa mkojo uliochanganyika na damu, kama vile mambukizi ya kwenye njia za mkojo na hata maambukizi ya baadhi ya magonjwa ya zinaa ikiwa yamedumu kwa muda mrefu bila tiba.

Lakini pia ikiwa unatoa mkojo uliochanganyika na damu, na hasa ukiambatana na maumivu ya mgongo au hata maumivu ya chini ya kitovu, hii ni ishara tosha kuwa unashambuliwa na baadhi ya maradhi ya figo na hasa uwepo mawe madogo madogo kwenye figo ambao kitaalamu tunaita kidney stones.

Tatizo hili hutokea wakati ambapo aina hii mawe yanajitengeneza na kujikusanaya kwenye figo baada mkojo kuchujwa na yale mabaki ya mkojo kutengeza mawe haya yatokanayo na ile chumvi chumvi.

Mawe haya hulazimika kutoka kupitia njia inayotumika na mkojo kutoka kwenye figo ndani hadi kwenye njia ya mkojo ya nje iliyoambatana na via vya uzazi.

Hivyo kupitia mchakato huu, wakati wingine mawe haya huchumbua njia ya mkojo wakati yakiwa yanalazimika kutoka nje na kusababisha majeraha madogo madogo kwenye njia ya mkojo na kutokwa na damu.

Ni vyema kumuona daktari ili kuangalia uwepo wa aina hii yam awe kwenye figo.

Lakini tatizo lingine kubwa, mkojo uliochanganyika na damu mara nyingi huashiria saratani ya kibofu, na hasa ikitokea huambatana na maumivu yoyote hivyo ni vyema kuwahi kupata vipimo ili kuliwahi tatizo hili katika hatua zake za awali.