Idadi ya watu waliokufa katika Ajali ya lori iliyogonga Magari mengine manne kabla ya kupinduka na kuwaka moto kwenye mteremko mkali wa Iwalanje, eneo la Igawilo jijini Mbeya imefikia 15, baada ya majeruhi wengine wawili kufariki dunia wakati wakipewa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya.

Muuguzi Mkuu wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda, Dk. Petro Seme amesema kuwa majeruhi wengine 13 wanaendelea na matibabu hospitalini hapo na kati yao wawili hali zao ni mbaya.

Ajali hiyo imetokea jana tarehe 07 Septemba, 2018 majira ya saa 10 jioni katika mteremko wa mlima wa Igawilo Jijini Mbeya baada ya Lori lililokuwa na shehena ya viazi, likitokea Tukuyu kwenda Mbeya Mjini kuyagonga magari matano likiwemo basi dogo lililokuwa na abiria.

By Jamhuri