Mmoja wa wataalamu akitoa huduma kwa mtoto mwenye  nyayo iliyopinda kwa kutumia njia ya Ponseti  katika Hospitali ya CCBRT Jijini Dar es Salaam.
Wataalamu wakiendelea kutoa huduma kwa wtoto wenye  nyayo zilizopinda kwa kutumia njia ya Ponseti  katika Hospitali ya CCBRT Jijini Dar es Salaam.
Excutive Director Miracle Feet, Chesca Colloredo akizungumza jambo.

HOSPITALI ya  CCBT ya Jijini Dar es Salaam kwa kushirikiana na Shirika lisilokuwa la kiserikali linalojishughulisha na kutoa huduma na matibabu ya nyayo za kupinda Tanzania( TCC0) wameendesha mafunzo ya wiki moja ya namna ya kutibu nyayo zilizopinda.

Huduma hiyo iliandaliwa pia kwa kushirikiana na wadau wa mradi wa mafunzo ya matibabu ya nyayo zilizopinda Afrika (ACT).

Mwenyekiti wa TCCO, Dkt. Robert Mhina akizungumza jambo.

Mafunzo hayo yanalengo la kujenga uwezo katika utoaji wa matibabu wa nyayo za kupinda ukanda wa kusini mwa jangwa la sahara kwa kutumia njia ya Ponseti, njia ambayo matibabu hutolewa bila kufanyika upasuaji.

Jumla ya washriki 65 wameshiriki mafunzo hayo wakiwemo wakufunzi maarufu wa matibabu ya nyayo zilizopinda duniani na wale wa kozi ya juu ya matibabu ya ulemavu huo, pia yametolewa mafunzo ya awali kwa wanaoanza kujifunza utaalamu huo.

Katika hotuba yake ya ufunguzi wa mafunzo hayo, Ofisa Mwendeshaji wa CCBRT, Brenda Msangi aliwakaribisha washiriki hao Tanzania, na kusema kuwa mafunzo hayo ni fursa ya pekee kwa CCBRT katika kuwaendeleza wataalamu wake wa ndani na hatua muhimu ya kujiimarisha kama kitovu cha mafunzo ya afya katika eneo la Afrika Mashariki.

“ Ili kuhakikisha idadi ndogo ya wataalamu wa afya walioko hapa nchini wanajengewa uwezo na nyenzo wanazozihitaji kutoa huduma bora kwa wagonjwa. CCBRT imeanzisha kituo cha mafunzo ya afya hapa Dar es Salaam na kitakuwa na mazingira ya hali ya juu ili kuwapatia ujuzi unaostahili wauguzi na wataalamu wengine wa afya,” alisema Brenda.

Kwa upande wake mmoja wa Madaktari Bingwa wa Upasuaji Mifupa CCBRT Dkt. Prosper Alute aliwataarifu washiriki wa mafunzo hayo akisema kuwa takribani watoto 2,200 Tanzania huzaliwa na nyayo za kupinda kila mwaka.

 

 

 

“CCBRT ni mtoaji mkubwa wa matibabu wa nyayo za kupinda hapa nchini na idara yetu ya mifupa inaowataalamu waliobobea katika kutoa matibabu ya nyayo zilizopinda kwa kutumia njia ya Ponseti na hii hutuwezesha kutibu watoto kama 400 hivi kwa mwaka . Lakini idadi hii bado ni ndogo ikilinganishwa na watoto wenye mahitaji, mafunzo kama haya yatasaidi kuziba pengo. Alisema Alute.

Aidha aliongeza kuwa mafunzo hayo ni muhimu sana kuendelea kufanyika katika Bara la Afrika ambapo inakadiriwa kuwa watoto wapatao 30, 000 wanazaliwa na nyayo zilizopinda kila mwaka, huku kukiwa na wataalamu wachache wa kuweza kutoa matibabu hayo.

By Jamhuri