Aliyekuwa daktari wa Donald Trump amesema kwamba si yeye aliyeiandika barua iliyomweleza mgombea huyo wa chama cha Republican wakati huo kuwa aliyekuwa na “afya nzuri ajabu”, vyombo vya habari Marekani vinasema.
“[Trump] alitunga na kuamrisha kuandika kwa barua yote,” Harold Bornstein aliambia runinga ya CNN Jumanne.
Ikulu ya White House haijazungumzia tuhuma hizo za daktari huyo.
Bw Bornstein pia amesema maafisa wa serikali walitekeleza “uvamizi” katika afisi zake Februari 2017 na kuondoa nyaraka zote zilizohusiana na taarifa za kimatibabu za Bw Trump.

Katika mahojiano na CNN, Bw Bornstein amesema barua hiyo ya mwaka 2015 iliyodokeza kwamba Bw Trump angekuwa “mtu mwenye afya bora zaidi aliyewahi kuchaguliwa kuwa rais” haikuwa utathmini wake wa kitaalamu wa hali yake ya afya.
“Nilitayarisha nilipokuwa nasonga,” anasema.
Haijabainika ni kwa nini Bw Bornstein anatoa tuhuma hizo kwa sasa.

Barua hiyo ilisema nini?

Barua hiyo ilikuwa na miongoni mwa mengine tamko kuhusu nguvu za kimwili za Bw Trump na ukakamavu wake, ambavyo vilielezwa kuwa “vya kipekee”.
Vipimo kuhusu shinikizo la damu yake na pia uchunguzi mwingine wa maabara vilielezwa kuwa “vya kushangaza kwa uzuri wake” na kwamba alikuwa amepoteza uzani wa kilo 7 katika kipindi cha mwaka mmoja.
Barua hiyo iliongeza kwamba Bw Trump hakuwa na aina yoyote ya saratani na hajawahi kufanyia upasuaji wowote wa maungo.

 

By Jamhuri