Mgombea urais wa chama cha Republican nchini Marekani, Donald Trump, amesisitiza kwamba Mexico italipia ukuta utakaojengwa mpakani kuzuia raia wake kuingia Marekani asilimia 100 iwapo atashinda urais.

Wakati wa hotuba yake muhimu kuhusu sera ya uhamiaji, Trump anasema atafutilia mbali uwezekano wa mamilioni ya wahamiaji wanaoingia nchini Marekani kinyume cha sheria watafurushwa iwapo ataingia mamlakani.

Baadaye akaoneka na kusisitiza msimamo wake mkali alipoongeza: “Kila mtu aliyeingia Marekani kinyume cha sheria anafaa kufurushwa…hii ndiyo maana ya kuwa na sheria. Hatuwezi kuwa watunga sheria halafu tukawa wavunja sheria.

“Wanaotaka kuingia Marekani wataulizwa maoni yao kuhusu mauaji, heshima kwa wanawake na wapenzi wa jinsia moja, na makundi ya wachache, na msimamo wao kuhusu Uislamu wa itikadi kali,” anasema Trump.

Ameuambia umati wa watu uliomshangilia sana katika jimbo la Arizona katika ziara yake nchini Mexico na kutilia mkazo kuwa atahakikisha ulinzi mpakani unaimarika kwa lengo la kuifanya Marekani kuwa kimbilio la watu wema kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.

Kuhusu sera yake ya uhamiaji, Trump pia anabainisha kuwa wale wote walioingia nchini Marekani kinyume cha sheria watafurushwa na kurejeshwa makwao kwa usalama wa Wamarekani wenyewe.

Saa chache kabla ya hotuba hiyo alikuwa amekutana na Rais wa Mexico, Enrique Pena Nieto, lakini akasema hawakuzungumzia ufadhili wa ujenzi wa ukuta huo anaotarajia kuujenga pindi tu atakaposhinda katika uchaguzi ujao.

Hata hivyo, Rais Pena Nieto, baadaye alisisitiza kwamba alimwambia Trump kuwa Mexico haitalipia ujenzi huo, lakini kumekuwa na uvumi kwamba  Ωhuenda mgombea huyo wa Republican akaamua kuachana na mpango wake wa kuwafurusha karibu wahamiaji 11 milioni walio Marekani kinyume cha sheria.

Anasema lugha anayotumia mgombea huyo wa urais wa chama cha  Republican Donald Trump ndiyo iliyowahi kutumiwa na madikteta wengi waliowahi kutokea hapa duniani kama  Adolf Hitler na Benito Mussolini na wengine wengi waliowahi kutokea hapa duniani.

Anasema hayo kwenye mahojiano na gazeti la ‘Excelsior’ na kuongeza kuwa matamshi ya kiongozi huyo yameathiri uhusiano kati ya Mexico na Marekani, kwa mujibu wa shirika la habari la ‘AP’.

Alipoulizwa kuhusu Trump, Pena Nieto alisema mambo ambayo mgombea huyo amekuwa akiyafanya na kuyapendekeza yamewahi kusababisha maafa makubwa katika historia. “Hivyo ndiyo Mussolini alijitokeza na ndivyo Hitler alivyojitokeza,” anasema Pena Nieto.

Pena Nieto alikuwa hajazungumza moja kwa moja kumhusu Trump ambaye ameahidi kujenga ukuta kati ya Mexico na Marekani ili kuzuia wahamiaji kutoka nchi hiyo wasiingie Marekani.

By Jamhuri