Huduma ya Kwanza: Shambulio la Moyo

Mwathirika wa ajali huhitaji ahudumiwe haraka, tena kwa muda mfupi, huku mipango ikiwa inafanywa hadi atakapotokea daktari au atakapopelekwa zahanati ama hospitali kwa tiba inayostahili…

 

Shambulio la moyo (heart attack) mara nyingi hufanana na kuzirai kunakompata mwenye msongo wa roho (asphyxiation) au aliyekosa hewa ya kutosha na hivyo kumletea maumivu ndani ya kifua na kwenye sehemu za juu tumboni. Wakati mwingine maumivu yake husambaa hadi mkono wa kushoto uliko moyo. Mlaze mgonjwa mahali penye ukimya, nguo zilegezwe shingoni, kiunoni na sehemu nyingine. Kama ataweza kunywa basi apewe chai au kahawa. Usichelewe kumwita daktari au kumpeleka hospitali. 

Msongo wa Roho 

Mtu aliyefunga pumzi au kupatwa na msongo wa roho (asphyxiation) atakufa kama hatasaidiwa ili aweze kuvuta pumzi. Sababu za kawaida za mtu kupatwa na tatizo hili zinatokana na kuvuta kwa wingi gesi mbaya ya carbon dioxide, kama ilivyo hewa ya kutoka mitamboni, kwenye makaa (hasa makaa ya mawe) yanayowaka. Vifo vingi vimetokea kwa watu wanaolala na majiko yanayowaka katika vyumba visivyokuwa na madirisha ya kutosha kutolea na kuingizia hewa vya kutosha. 

Pia mtu anaweza akapatwa na shida hii kutokana na kugusa waya au chombo chenye nguvu ya umeme (live electric current) au kutokana na kuvuta hewa yenye sumu za aina nyingine, pamoja na kutumia kwa wingi kupita kiasi dawa za kutuliza maumivu (sedatives). 

Mtu akipatwa na tatizo la kukosa hewa, mara moja afanyiwe huduma ya kumwezesha kuingiwa na hewa mapafuni (artificial respiration). Fanya hivyo mara baada ya kumwondoa mahali alipo na kumweka sehemu ya wazi, penye hewa. Waokoaji wanaoingia penye moshi au hewa yenye sumu, lazima wahakikishe wamevaa vifaa maalum (life line) vya kuwazuia wasivute hewa hiyo kwa wingi. Kazi hii yahitaji kufanywa na watu wengi.

Kiharusi 

Kiharsui ni ugonjwa unaomjia mtu ghafla ubongoni, kiasi kwamba hataweza kumudu kutumia viungo vyake wala hatakuwa na hisi za mguso (sense of touch). Atakuwa na kifafa akifurukuta mikono na miguu na kujipindapinda (convulsion). Inabidi alazwe chali, mabega na mikono yake ikiwa imeinuliwa na afunikwe vyema. Mfuko wa maji baridi ama barafu husaidia ikiwekwa kichwani. Asipewe kileo, dawa ama kitu chochote kinachoweza kuusisimua (stimulants) mwili wake. Asitikiswe ama kubughudhiwa.   

Majeraha ya Risasi

Majeraha ya risasi za bunduki na bastola (gunshot wounds) huingia ndani sana mwilini na kuifanya damu ivuje ndani kwa ndani, ama katika viungo (glands) vya ndani ya mwili (internal haemorrage). Mshituko wa kurukwa na damu (shock) huwa ni jambo la kawaida kwa mtu kama huyo na lazima apelekwe hospitali haraka. 

Majeraha ya Tumboni

Hatari ya majeraha yanayotokea ndani ya eneo la tumbo (wounds of abdomen) ni kwamba yanaweza yakawa yametoboa utumbo au kiungo kingine cha ndani ya tumbo. Kwa nje ya mwili, kwa kawaida, jeraha lake huwa halionekani. Mtu anayejeruhiwa tumboni lazima apelekwe hospitakli haraka.

Kuumwa na Tumbo

Maumivu kutoka ndani ya tumbo (abdominal pain) huwa ni dalili ya kuwapo kwa hitilafu mwilini — nyingi zikiwa za hatari zaidi ya nyingine. Wakati mwingine tumbo huuma mtu akiwa na ugonjwa fulani ndani ya mfuko wa tumbo (stomach), au kutokana na tatizo la kwenda haja, kufunga choo, au kama anaharisha.

Maradhi ya appendicitis – kule kuvimba kwa kichango cha utumbo kilicho kama ncha kilichojitokeza nje ya utumbo (appendix) yanaweza yakaanza yakiwa yanaambatana na maumivu kwenye sehemu za chini kuliani mwa tumbo, si mbali sana na kiunoni. Homa inaweza ikawapo kidogo ama isiwepo kabisa.