Waanza zengwe la tatu bora
Kinana akata mzizi wa fitina

 

 

Taarifa kuwa Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa, huenda akaenguliwa iwapo atatangaza nia na kuchukua fomu kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, zimezidi kushika kasi.

Lowassa hajatangaza kuwania nafasi hiyo ya juu kabisa katika utumishi wa umma nchini, lakini harakati zake za siasa pamoja na watu wake wa karibu zinaonesha kuwa Mbunge huyo wa Monduli kwa zaidi ya miaka 20, huenda akawa mgombea.

Umeundwa pia mtandao unaosambaza taarifa kuwa Lowassa anaumwa, ukitaraji kuwa umma utafika mahala utaamini maneno hayo, ambayo yamesemwa mara kadhaa, na Lowassa akajitokeza hadharani akiwa mwenye siha njema.

Mmoja wa viongozi wa CCM, ameieleza JAMHURI kwamba Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, yuko njiapanda kutokana na shinikizo la kuchuja wagombea Aprili, mwaka huu akiwamo Lowassa.

Mtoa taarifa amesema hatari kubwa iko kwa vigogo watatu ambao baadhi yao wametangaza nia. Vigogo au makada hao kwa sasa wanapigiwa chapuo waingie hatua ya tatu bora ndani ya CCM, na hapo ndipo wanapopambana Lowassa asifikie.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohamed Gharib Bilal, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ambaye tayari ametangaza ‘kimyakimya’, nao wanatajwa kumtesa Rais Kikwete.

“Hili linamuumiza kichwa Mwenyekiti (Rais Kikwete). Kwa kweli yuko njiapanda. Watu anaofanya nao kazi anawatosaje? Yeye mwenyewe halisemi hili ovyo. Ni gumu na linalosumbua kichwa,” anasema mtoa habari na kuongeza.

“Kuna mashinikizo ya kuwafikiria anaofanya nao kazi kwa sasa, Makamu wa Rais amefanya naye kazi kwa kipindi chote cha miaka mitano; Waziri Mkuu atamtosa vipi, rafiki yake Membe atamtoa vipi?” anahoji mtoa taarifa.

“Hawa ni lazima wapite, kwa sababu taarifa zinasema kama Lowassa akipenya tu ndani ya tatu bora, ujue atateuliwa. Mbinu hapa ni kufanya asifike huko,” anasema mtoa taarifa huyo aliyeomba kuhifadhiwa jina.

Lowassa hajatangaza kuwania nafasi hiyo, ila karibu kila kona ya nchi hii mazungumzo ya wananchi wa kawaida wanasema wazi kuwa wangetaka Lowassa apewe usukani aweze kunyoosha mambo yaliyopinda kutokana na falsafa yake ya kufanya uamuzi mgumu kwa wakati bila kuremba.

Bernard Membe kwa upande wake, ingawa ametangaza tayari kutogombea ubunge katika Jimbo la Mtama, ambapo Katibu wa Uenezi na Itikadi wa CCM, Nape Nnauye, amejipanga kugombea jimbo hilo, kuhusu urais, anasema hadi sasa “hajaoteshwa.”

Makamu wa Rais, Dk. Bilal mwishoni mwa mwaka jana wakati Rais Kikwete anaumwa alikutana na wahariri kwa chakula cha jioni nyumbani kwake, na wahariri walipomhoji iwapo atagombea urais, maana wakati huo alikuwa Kaimu Rais, Rais Kikwete alipokuwa Marekani kwa matibabu, wasaidizi wake walijibu kwa niaba yake kuwa hawajasikia neno la aina hiyo kutoka kwake. Yeye hakujibu neno hilo, badala yake akapiga picha na wahariri wakatawanyika.

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, yeye alipohojiwa na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) iwapo ana nia ya kugombea urais, alimjibu Salim Kikeke, ambaye ni Mtangazaji wa BBC kuwa yeye bado anatangaza “kimyakimya.”

Mbinu nyingine inayopendekezwa kutumiwa kukata jina la Lowassa ni kuendelezwa kwa adhabu dhidi ya kada huyo pamoja na makada wengine watano ambao mwaka mmoja uliopita, waliadhibiwa na chama kutokana na kasi ya kuonesha nia ya kuwania urais.

Makada wengine walioadhibiwa na Lowassa ni Membe, Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uhusiano), Stephen Wasira, Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia, January Makamba, na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.

Licha ya makada hao kufungiwa mwaka mmoja kuanzia Februari 18, mwaka jana kutojishughulisha na shughuli za kisiasa kwa kuwa zingewapa kura ya turufu katika kuwania uongozi wa nchi, baadhi yao hawakujali kwani waliendelea kutangazani nia.

Viongozi hao waliadhibiwa na Kamati Ndogo Maalum ya Nidhamu iliyowatia hatiani kwa kosa la kuanza kampeni mapema. Kamati hiyo iliongozwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM, Philip Mangula.

Hata hivyo, Makamba, Wasira na Sumaye wameendelea na shughuli za kijamii bila hofu, huku wengine wakijitokeza akiwamo Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba; Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Asiye na Wizara Maalum, Profesa Mark Mwandosya, na Mbunge wa Nzega, Dk. Hamisi Kigwangalla.

Mtoa taarifa anasema tahadhari kubwa ya Rais Kikwete ipo katika kutengeneza uhusiano na diplomasia ndani ya chama kwamba baada ya uteuzi kusiwe na mgawanyiko aina yoyote.

Mtoa habari ambaye ametoka kwenye vikao vya CCM huko Zanzibar amesema kwa nia ya kujenga uaminifu kwenye chama na Serikali, anasema Rais Kikwete anapata taabu kutokana na Lowassa kuwa na sifa mbili kwake.

Kwanza Rais Kikwete anawaza uhusiano kati yake na Lowassa walioutangaza kwamba “hawakukutana barabarani”, na pili nguvu ya ushawishi na Lowassa kuungwa mkono na wanachama wengi na hata nje ya chama. Licha ya Lowassa kutotangaza nia, lakini waliotangaza nia, kauli zao zinaonesha kutaka kupambana na mbunge huyo ambaye CCM ilifikia hatua ya kumpunguza kasi yeye na makada wenzake watano mwaka jana.

Taarifa zinasema kwa mara ya kwanza wakati Rais Kikwete anaingia madarakani, alikubali kupewa Makamu Rais aliyekuwa Mgombea Mwenza, Dk. Mohamed Shein lakini akapinga kuletewa Waziri Mkuu. Nafasi hiyo alimpa kada mwenzake wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mbunge wa Monduli Lowassa ambaye alikitumikia cheo hicho kwa miaka miwili na mwezi mmoja kabla ya kujiuzulu akateuliwa Pinda.

Abdulrahman Kinana, Katibu Mkuu wa CCM ameiambia JAMHURI kuwa chama hakina mpango wa kumtimua mwanachama yeyote kama inavyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari.

Lakini akasisitiza, “CCM itakuwa makini sana na mgombea atakayeteuliwa. Katika hili la urais na uchaguzi wa wabunge na madiwani, chama kiko makini sana katika haya. Sawa.”

Mchakato wa uchaguzi ndani ya CCM unatarajiwa kukamilishwa Aprili, mwaka huu. Hii ina maana mwezi Machi utakuwa mwezi wa mikikimikiki. Wagombea watarajiwa karibu wote hawakuwa tayari kulizungumzia hili, wakiiambia JAMHURI kuwa wakati haujawadia.

By Jamhuri