Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo akitoa salamu zake za maadhimisho ya Wiki ya Sheria.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (wa tatu kutoka kulia) akiwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Sumbawanga John Mgeta (wa kwanza kushoto) na Jaji Mkuu wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Sumbawanga Dk. Adam Mambi (wa pili kutoka kulia) na Mwanasheria wa Serikali mkoa wa Rukwa Prosper Regerera.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo akisalimiana na Jaji Mkuu wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Sumbawanga Dk. Adam Mambi.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo amesema maboresho ya TEHAMA yanayofanywa na mhimili wa mahakama nchini utasaidia kupunguza foleni za wananchi wanaofika ofisi za Wakuu wa Wilaya na kwa Mkuu wa Mkoa kutafuta haki zao.

Amesema kuwa kitendo cha mwaanchi kuweza kujua mwenendo wa kesi bila ya kufika mahakamani ni maendeleo makubwa yanayofikiwa na mhimili huo na kuwaasa kuanza kufanya kazi baada ya kuwa likizo ya mwisho wa mwaka.

Ameyasema hayo kwenye maadhimisho ya wiki ya sheria ambayo hufanyika tarehe 1, Februari ya kila mwaka katika Viwanja wa mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Sumbawanga inayojumuisha mikoa ya Rukwa na Katavi.

“Mwaka 2018 na jitihada zilizofanyika na mahakama umekuwa mwanzo mzuri, wananchi watajitokeza kutafuta elimu hii ya sheria na wanapoipata itatupunguzia msongamano kwenye ofisi zetu za Mkuu wa Wilaya na Mkuu wa Mkoa ili tufanye kazi za maendeleo sio kusuluhisha migogo ya ndoa, mirathi na ardhi ambayo yote imekaa katika misingi ya kisheria,” Alieleza.

Na kuongeza kuwa elimu hii ya sheria iendelee kutolewa ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wakati huku wakizingatia kaulimbiu ya maadhimisho hayo inayosema “Matumizi ya TEHAMA kwa kutoa haki kwa wakati na kuzingatia maadili.”

Kwa upande wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Sumbawanga John Mgeta ametahadahrisha matumizi mabaya ya Teknolojia katika kuvunja maadili na misingi ya mahakama na utu kwani watu hutumia teknolojia hiyo kuendeleza rushwa kupitia namba za simu za mahakama.

“Mtumishi wa mahakama anaweza kutumia simu kuwasiliana na mtu akimuomba rushwa au kufanya miamala ya pesa, vyombo vya habari na wananchi ambao wanakiuka maadili kwa kutumia simu na TEHAMA, sisi tunasisitiza matumizi haya yazingatie maadili,” Alibainisha.

Awali akitoa taarifa ya chama cha wanasheria Tanzania Wakili Baltazar Chambi amesema kuwa mahakama ya Tanzania kwa kutumia TEHAMA itafikia suluhu mojawapo ya uhakika wa utoaji wa haki kwa wakati kwa kulitambua hilo wadau wa haki ni vyema wakajua matumizi ya TEHAMA ili kuleta ufanisi katika kazi zao.

By Jamhuri