Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt Harrison Mwakyembe ameeleza kufurahishwa na mchezo wa Kombe la Shirikisho Africa kati ya Simba SC na Gendarmerie ya nchini D’jbout ambapo Simba iliibuka kidedea kwa kuichapa timu hiyo mabao 4 – 0, mechi iliyochezwa katika uwanja wa taifa Dar es Salaam.

Waziri Mwakyembe alieleza kuwa kwa kiwango cha soka kilichoonyeshwa na timu ya Simba, kinadhihirisha kuwa wamejipanga na wana mafunzo mazuri kutoka kwa kocha wao na kama wataendeea hivyo, basi kiwango cha soka Tanzania kitazidi kukua maradufu.

“Nimebahatika kuiona mechi ya leo, ilikuwa ni mechi nzuri sana. Unaiona Simba kama timu ambayo kweli ilikuwa kambini, ina mwalimu, ina uelewano wa hali ya juu. Mchezo ulikuwa mzuri sana. Nimefurahia na kama kiwango cha mchezo wa mpira Tanzania kitakuwa hiki, kama alivyosema Mzee wetu Ally Hassan Mwinyi sisi siyo tena kichwa cha mwenda wazimu ila kichwa cha muungwana ambacho kila mtu lazima akisogelee kwa uangalifu sana,” alisema Waziri Mwakyembe.

Akizungumzia kuhusu malalamiko yaliyotolewa na timu ya Yanga kuhusu kunyimwa nafasi ya kufanya mazoezi katika uwanja wa Taifa siku moja kabla ya mchezo, Waziri Mwakyembe alieleza kuwa kutokama na ukarabati wa uwanja huo uliofanyika mwaka jana, masharti yake ni kuchezewa mechi zisizozidi tatu tu kwa wiki na tayari mechi hizo zilikuwa zimeshachezwa.

“Kuhusu Yanga kulalamika, sisi hatujayapata malalamiko rasmi ya Yanga yenyewe, nimeyasikia Bungeni watu wakiyasema, lakini cha msingi ni kwamba wote mnajua uwanja wetu wa taifa umetoka katika ukarabati mkubwa sana. Tumekabidhiwa ukiwa na garantee ya kuweza kutumia huo uwanja kwa zaidi ya miaka kumi bila kuweka nyasi mpya. Lakini una masharti yake, huwezi ukawa na michezo mitatu kwa wiki katika uwanja huu. Ukifanya hivyo hatuwezi kuwa na uwanja huu katika miaka miatu ijayo,” alisema.

Waziri Mwakyembe aliongeza kuwa waliwapa kipaumbele timu ya wageni kufanyia mazoezi katika uwanja huo, kwa kuwahawakuwa wanaujua uwanja na hiyo ndiyo fursa yao ya kuuzoea, jambo ambalo linatambulika kimataifa katika utaratibu wa michezo.

“Katika mechi ya kimataifa, timu ngeni inapewa kipaumbele kuweza kufanya mazoezi kwenye uwanja uleule ambao ni uwanja wa wenyeji. Kwa hiyo kwa upande wa simba na Yanga, huu ni uwanja wao, inachukuliwa wanaujua. Wale ni wageni hawaujui uwanja wao. Kwa hiyo sisi tulivyoona ukiwapa wote wakafanya mazoezi hapa, utakuwa na mechi saba katika uwanja unaoruhusiwa mechi tatu tu. Kwa hiyo ilibidi sisi tuwape wageni priority ili waweze kufanya mzoezi kwenye kiwanja hiki,” alieleza.

Hata hivyo Waziri aliwashauri Yanga kuahana na malalamiko na badala yake wapambane kufanya mazoezi kwa ajili ya mechi zinazokuja kwani ushindi wao ni ushindi wa taifa kwa ujumla.

“Niwashauri Yanga kwamba akili yao yote ikazanie mechi ya marudio inayokuja, waaache mambo ya kulalamika lalamika. La msingi akili yao yote iwe katika mechi inayokuja. hakuna dawa, hakuna mwarobaini wa kushinda ni mazoezi na timu kuweza kuelewana,” alisisitiza.

By Jamhuri