WAZIRI wa Mambo ya Ndani, Dkt. Mwigulu Nchemba ameliagiza Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi kina kuhusu tukio la mauaji ya aliyekuwa Katibu wa CHADEMA Kata ya Hananasif, Daniel John yaliyotokea Kinondoni jijini Dar es Salaam na matukio mengine ya mauaji yanayotokea hapa nchini.

Mwigulu amemuagiza Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Simon Sirro na timu yake kufanya uchunguzi wa kina juu tukio hilo na kujua undani wake ni nini huku akiwataka kuwataarifu wananchi nini kinachoendelea dhidi ya tukio hilo na mengine ambayo yamekuwa yakiripotiwa.

Mwigulu ametoa maagizo hayo akiwa mkoani Kagera wilaya ya Muleba katika Kata ya Kasindaga wakati wa uzinduzi wa uandikishaji wa vitambulisho vya Taifa mkoani humo.

“Mataifa mengine mtu akiuwawa shughuli zote zinasimama, tusiweke haya mazoea ya watu wanapotepotea kama mtu kapuliza dawa ya mbu. Kama jambo la kawaida tu, wafanye uchunguzi kwa kina kujua nani amehusika na tukio hili. Masuala ya demokrasia huamuliwa kwa peni na karatasi na si kwa panga, lungu wala mkuki,” alisema Waziri Mwigulu.

By Jamhuri