Udumavu wa kufika kileleni: Huu ni upungufu wa nguvu za kiume. Ni hali ya kufika kileleni ambayo hutokea kwa polepole sana au kushindwa au kutokuwa na uwezo kabisa wa kufika kileleni kutokana na ukosefu wa shahawa.

Ufikaji kileleni unaorudi: Huu pia ni upungufu wa nguvu za kiume. Ni hali ambayo ule mshindo wa raha (unaotokana na ufikaji kileleni) hulazimishwa kurudi na kuingia katika kibofu cha mkojo.

Uume kutosimama vizuri (kusimama kwa ulegevu): Huu ni upungufu wa nguvu za kiume. Ni hali ya kukosa uwezo wa kusimamisha uume au kudumisha usimamishaji huo wa uume katika kiwango bora cha kutosheleza tendo la ndoa.

Kukosa hamu ya tendo la ndoa: Huu ni upungufu wa nguvu za kiume. Ni hali ya mtu kutokuwa na hisia za kufanya tendo la ndoa. Moyo unatamani kutenda tendo la ndoa lakini hamu hakuna! Ni kama mgonjwa ambaye ana njaa lakini hana hamu ya kula, hata kama angewekewa vyakula vizuri vizuri kama mayai, kuku, samaki waliopikwa  au kukaangwa vizuri na kadha wakadha; atakwambia, “Sina hamu kabisa ya kula, nahitaji uji tu wenye  limao!”

Kushindwa kurudia tendo la ndoa: Huu ni upungufu wa nguvu za kiume. Ni hali ya kushindwa kurudia tendo la ndoa ‘round’ ya pili. Hiki nacho ndicho kilio cha wanaume wengi hivi leo. Baada ya tendo la ndoa la mara ya kwanza hawezi kurudia tena mara ya pili au anachukua muda mrefu sana kurudia. Au anachoka sana, hamu inakufa kabisa kiasi hata cha kuchukia tendo lenyewe la ndoa.

Kukosa nguvu au pumzi ya kusukuma: Huu pia ni upungufu wa nguvu za kiume. Ni hali ya kukosa nguvu au pumzi ya kusugua au kusukuma. Mtu anachoka, hawezi hekaheka za kitandani!

Kushindwa kufanya mitindo tofauti tofauti: Huu pia ni upungufu wa nguvu za kiume. Ni hali ya mtu kushindwa kufanya staili mbalimbali za mapenzi kutokana na hali au matatizo ya mwili wake.

Kuhisi hofu au maumivu sehemu za siri na sehemu nyinginezo: Huu ni upungufu wa nguvu za kiume. Kuna wanaume kabla ya tendo la ndoa anakuwa na hofu sana, na anapofika katika tendo lenyewe anakuwa hawezi kabisa! Wanaume wengine huhisi maumivu katika uume au korodani au kiuno, au sehemu yoyote nyingine ya mwili wakati wa tendo la ndoa au baada ya tendo la ndoa au hata kabla ya tendo la ndoa.

Ndugu msomaji, hivyo ni baadhi ya vipengele vya upungufu wa nguvu za kiume. Ni vingi sana. Kwa ufupi tu ni kwamba iwapo moja ya matatizo niliyoyataja hapo juu au zaidi yatakutokea, jifahamu wazi kwamba una upungufu wa nguvu za kiume, na hivyo sasa ni muda mwafaka wa kutafuta matibabu sahihi bila kuchelewa.

Mtu aelewe ya kwamba anapojitibu mapema anakuwa anajitengenezea fursa pana ya kupona, kwa sababu ubaya wa tatizo hili, kadiri siku zinavyokwenda ndivyo pia ugumu wa matibabu unavyokuwa mkubwa zaidi, viungo vilivyoathirika vinakuwa vikorofi zaidi kuitika dawa kutokana na ugonjwa kuwa sugu. Wahenga walisema: “Chelewa chelewa utakuta mwana si wako!”

Jinsi uume unavyosimama na mtu kufika kileleni

Ili kuelewa vizuri upungufu wa nguvu za kiume, kwanza kabisa tunapaswa kuelewa sayansi ya tendo la ndoa, jinsi uume unavyosimama na jinsi mtu anavyofika kileleni (yaani anavyomwaga manii); hapo sasa itakuwa rahisi msomaji kuelewa kiungo gani, au mfumo gani au kitu gani, ndani ya mwili kilichokorofisha.

Viungo vya tendo la ndoa kwa mwanaume ni uume, korodani, urethra na tezi-shahawa [prostate gland]. Urethra ni mrija wa kupitishia mkojo kutoka kibofuni hadi kwenye uchi wa kiume au wa kike; pia ni mrija ambao hutumika kupitishia shahawa. Na tezi-shahawa ni tezi ya homoni ya sehemu za kiume za uzazi wa mamalia zinazosaidia kuunda manii.

Uume umeundwa na mirija mitatu yenye uwazi au nafasi tatu zinazosababisha usimamaji wa uume. Damu huingia kwenye mirija miwili wakati wa msisimko wa mapenzi ili kuufanya uume usimame. Mirija hii huitwa Corpora cavernosa. Ni tishu ya sponji ambayo iko kama puto, hutanuka na kusinyaa. Damu inapoingia ndani yake hutanuka na hapo uume husimama, na damu inapotoka ndani yake husinyaa, na hapo uume hulegea.

Mirija hii huanzia kwenye mfupa wa nyonga na kutanuka hadi chini kidogo ya kichwa cha uume, imeundwa na misuli laini na mishipa ya damu. Msisimko wa mapenzi husababisha mirija hii [corpora cavernosa] kujaa takribani 100-140 ml za damu na kadiri zinavyovimba, ndivyo uume unavyosimama.

Urethra ni mrija wa tatu, ambao huanzia kibofuni na kuendelea hadi kwenye ncha ya uume, unapita chini ya mirija hii miwili. Vyote viwili — mkojo na shahawa — husafiri kupitia urethra na kutoka ndani ya mwili. Korodani huzalisha na kutunza baadhi ya mbegu (shahawa), huku tezi-shahawa ambayo kwa jina jingine huitwa tezi-dume, ikitengeneza maji ambayo hubeba shahawa.

By Jamhuri