Septemba 11: Tukio lisilosahaulika Marekani

nmb-4Dunia imetimiza miaka 14 tangu kutokea mashambulizi ya kigaidi yaliyofanywa na Al-Qaeda.

Mashambulizi hayo yalitokea saa 2:00 asubuhi Jumanne, Septemba 11, 2001 ambako watu 19 waliokuwa ndani ya ndege nne za kuvuka mabara (Trans – Continental Flights) kuziteka na kuzigeuza kuwa silaha za maangamizi zikibamiza Kituo cha Biashara (World Trade Centre) New York, Marekani.

Haya yalikuwa ni madhara dhahiri ya ugaidi ambayo kamwe hayawezi kusahaulika wala kufutika katika akili za Wamarekani na dunia kwa ujumla. Licha ya tukio lile kuua watu wote waliokuwa ndani ya zile ndege, idadi ya watu waliokuwa katika jengo lile isiyojulikana bila kujali uraia wao waliuawa pale pale.

Makala hii inapembua kikamilifu juu ya asili ya ugaidi wa kikundi cha Al-Qaeda ambacho kilitekeleza azima hiyo; na kimsingi makovu yake yanajidhihirisha hata Tanzania na sehemu nyingine duniani bila kusahau majirani zetu Wakenya. 

Makala hii inajikita katika kuchunguza madai ya ugaidi wa kimataifa katika kutekeleza azima hiyo.

Tutakumbuka madhara ya ugaidi katika Balozi za Marekani (Dar es Salaam) na kule Kenya (Nairobi) ambako watu walipoteza maisha na palitokea uharibifu mkubwa wa mali na majengo yenye thamani kubwa 1998.

Mashambulizi ya kigaidi ya ‘Twin Towers – yaani ghorofa pacha’ yaliangamiza watu takribani 3,000; Al-Qaeda ikihusika moja kwa moja. Hili ni jambo lisilofichika ya kwamba ugaidi umeleta hofu na madhara yaliyodhahiri miongoni mwa jamii duniani.

Kila binadamu, katika muktadha huu amekuwa mhanga mtarajiwa wa matukio ya ugaidi. Vikundi chipukizi vyenye itikadi kali kama vile Al-Shabaab, Boko Haram, Anti Balaka, Sekela na kadhalika ni matokeo ya imani kali ikiwa na dhamira moja ya kutenda uovu ama kulipa kisasi dhidi ya mamlaka fulani kama njia waliyojichagulia kupenyeza sauti zao juu ya matakwa/madai fulani fulani.

Na wakati mwingine vikundi hivi vimejinasibisha kuwa na mahusiano au mafungamano na kikundi cha kigaidi cha Al-Qaeda ambacho kiliasisiwa na Osama Bin Laden.

Na pengine kuna mawazo potofu miongoni mwetu ya kwamba madhali gaidi huyo nambari moja duniani alishauawa, ugaidi utapungua au kukoma, ni vema tukatambua ya kuwa katika hali halisi ugaidi ni itikadi, na itikadi huwa haifi abadani. Kwa namna nyingine Osama Bin Laden ni taasisi tosha, tunapomchambua hatumwangalii kama mtu binafsi bali kama taasisi.

Lakini kabla hatujazama katika hadidu rejea za hapo juu, ni vema tukaliangalia na kujikumbusha lile tukio la kihoro lilivyotokea hiyo Septemba 11 angalau jinsi moja ya zile ndege nne ilipogeuzwa kuwa silaha ya maangamizi kwa mujibu wa Ripoti ya Tume ya Septemba 11 (The 9/11 Commission Report) iliyoandikwa na maseneta 15 kutoka Republican na watano kutoka Democratic chini ya Mwenyekiti wake, Thomas H. Kean. 

Ilikuwa ni Jumanne, Septemba 11, 2001, hali ya hewa ikiwa ni ya joto, mawingu kiasi mashariki mwa Marekani. Mamilioni ya wake kwa waume wakijiandaa kwa ajili ya kazi, wengine wakielekea katika lile jengo la ghorofa pacha (Twin Towers) la na Kituo cha Biashara cha Kimataifa (World Trade Centre), kwenye jiji la New York. 

Wengine walielekea Arlington, Virginia Pentagon katikati mwa mto Potomac, Bunge la Congress lilikuwa limerejea kwenye kipindi (session). Katika ule mtaa maarufu wa Pennsylvania watu walikuwa wameanza kupanga msuruhu kwa ajili ya ziara ya White House.

Kwa wale ambao walikuwa wakielekea uwanja wa ndege, hali ya hewa haikuwa salama na bora kwa safari. Miongoni mwa wasafiri alikuwamo Mohamed Atta na Abdul Aziz Al Omar, waliowasili katika Uwanja wa Ndege wa Portland Maine.

Ndani ya Ndege nne

Atta na Omari walipanda ndege saa 12 alfajiri, ndege kutoka Portland kuelekea Uwanja wa Boston Logan. Baada ya kuwa amekagua mzigo wake tayari kwa kupanda ndege, Atta alibainiwa na mfumo unaojulikana kwa kitaalamu CAPPS (Computer Assisted Passenger Prescreening System), uliotengenezwa kwa minajili ya kubaini wasafiri ambao wanapaswa kufanyiwa uchunguzi maalum kwa ajili ya hatua mahususi za kiusalama.

Chini ya kanuni za kiusalama katika kipindi ambacho tukio la Atta kuchunguzwa na kile kifaa maalum, begi la Atta lilizuiwa hadi hapo itakapothibitishwa pasi na shaka. Hata hivyo, mchakato ule haukuzuia mipango ya Atta.

Atta na Omar waliwasili Boston saa 12:45 dakika saba wakiwa wamechelewa. Baada ya muda, Atta alipokea simu kutoka kwa Marwan Al Shehhi, rafiki yake wa muda mrefu aliyekuwa katika uwanja mwingine wa Logan walizungumza kwa dakika tatu, na yale yalikuwa ni mazungumzo yao ya mwisho.

Kati ya saa 12:45 na saa 1:40, Atta na Omar wakiwa pamoja na Satam Al Suqami, Wal al Sherri na Waleed al Shehri walithibitisha usafiri (check in) na kupanda Ndege ya American Airlines kuelekea Los Angeles. Ndege ilipangiwa kuondoka saa 1:45

Katika uwanja mwingine wa Logan, Shehhi aliungana na Fayed Banihammad Mohand al Shehri, Ahmed al Ghamdi na Hamza al Ghamdi, wakipanda Ndege ya United Airlines nambari 175 kuelekea Los Angeles. Marafiki wengi wa Shehhi hawakuwa wazoefu wa masuala ya safari kwa mujibu wa wakala wa tiketi ya United Airlines. Ndege yao ilipagwa kuondoka saa 2.

Vizuizi vya usalama (security check points) ambavyo wasafiri akiwamo Atta na washirika wake, vilipata udhibiti madhubuti katika lango Na. 11 chini ya ulinzi wa Globe Security iliyoingia mkataba na American Airlines katika viwanja tofauti.

Kizuizi cha usalama ambacho usafiri wa Shirika la United walipita kilidhibitiwa na ilikuwa imeingia mkataba na Huntleigh USA kufanya upekuzi (screening).

Katika kupitia kwenye vizuizi hivi, kila mtekaji angechekechwa kupitia kifaa kinachoitwa Walk through Metal detector ambayo angalau vina mchanganyiko wa metali ya 22 calibre hand gun. Yeyote ambaye angekuwa amewekwa kile kingamuzi angekuwa amechekechwa na kifaa kile, mchakato ambao mpekuzi angeweza kubaini vitu vyenye asili ya chuma na punde kifaa kingetoa mlio fulani.

Zaidi ya hapo, mashine ya X-ray ingechekecha watekaji pamoja na mizigo yao ya mikononi. Mchakato ule ungewezesha kupokonywa silaha watekaji ikiwa ni pamoja na vitu vingine ambavyo mtu haruhusiwi kuwa navyo katika ndege za biashara. Hakuna wasimamizi wowote katika vizuizi walioripoti kitu kilichotilia shaka katika jambo zima la upekuzi.

Wakati Atta alikuwa ameshakuwapekuliwa na kifaa kiitwacho CAPPS pale Portland, washirika watatu ambao walikuwa kwenye timu ya utekaji Suqam, Wail al Shehri na Waleed al Shehri walikuwa wamefanyiwa upekuzi kule Boston. Upekuzi ule uliathiri tu mizigo yao ya mikononi, lakini haikuathiri chochote katika kizuizi cha usalama. 

Washirika wote watano walikuwa wamefanyasha pitishwa (cleared) katika vizuizi na wakaendelea na safari yao katika geti la American 11. Atta, Omar na Suqami walipata viti katika daraja la Business kiti namba 8D. 8G na 10b. Kina Shehri walikuwa mkabala mstari wa pili (2A na 2B) chumba cha daraja la kwanza walipanda ndege America 11 kati ya saa 1:31 na 1:40 – ndege ilianza kupaa saa 1:40:9/

Shehhi na timu yake hawakufanyiwa upekuzi/uchunguzi na kifaa cha CAPPS, wakipanda ndege ya United 175 kati ya saa 1:23 na 1:28 (Banihamad 2A, Shehri 2B, Shehhi 6C, Hamza Al Ghamdi 9C na Ahmed Al Ghamdi 9D) ndege yao iliondoka kabla ya saa 2:00