Januari 11, mwaka huu, mashabiki wa soka na Watanzania kwa jumla wataelekeza macho na masikio yao mjini Adis Abab, Ethiopia, wakati Taifa Stars itakapojipima nguvu na wenyeji wao.

Ethiopia inajiandaa kwa ajili ya michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika yanayotarajiwa kuanza kutimua vumbi Januari 19, mwaka huu nchini Afrika Kusini.

 

Matarajio ni kwamba Taifa Stars imejiandaa kutumia nafasi hiyo vizuri ili kuwapa raha mashabiki na Watanzania kwa jumla.

 

Watanzania tuna kila sababu ya kujivunia mtanange huo kwani ni fursa nzuri kwa timu yetu hiyo kujipima umahiri wake wa kisoka dhidi ya Ethiopia yenye kiwango kinachoridhisha katika soka.

 

Tayari Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura, amesema maandalizi ya wachezaji wa Taifa Stars kwa ajili mchezo huo yamefanyika vizuri.

 

Kauli hiyo ya Wambura inawapa matumaini mashabiki na Watanzania kwa jumla kiasi kwamba hawatarajii siku hiyo kuona na kusikia wachezaji wa Taifa Stars wakiondoka uwanjani midomo wazi, mikono kichwani na kuinamisha nyuso.

 

Matumaini ya wengi ni kwamba wachezaji wa Taifa Stars wameshajua matarajio makubwa waliyonayo Watanzania, hivyo watawaezi kwa kuhakikisha wanaibuka na ushindi mnono katika mchuano huo.

 

By Jamhuri