President-elect Obama with Nancy Killefer, the new Chief Performance Officer, for his administration. The news conference held at the transition office in Washington, D.C. on Jan. 7, 2009. President-elect Obama with former Presidents Bush (41), Carter and Clinton and current President Bush at the WHite House on Jan. 7, 2009. (Photo by Pete Souza)
President-elect Obama with Nancy Killefer, the new Chief Performance Officer, for his administration. The news conference held at the transition office in Washington, D.C. on Jan. 7, 2009.
President-elect Obama with former Presidents Bush (41), Carter and Clinton and current President Bush at the WHite House on Jan. 7, 2009.
(Photo by Pete Souza)
Wakati kampeni za kuwania kiti cha Urais ndani ya Taifa kubwa na tajiri la Marekani zikiendelea kupamba moto tayari mgombea asiyeishiwa vituko wa chama cha Republican  Donald Trump amemtaja mshindani wake wa chama cha Democrat Hillary Clinton kuwa ‘shetani’.

 Akizungumza kwenye mkutano huko Pennsylvania bwana Trump pamoja na kumshambulia Clinton vilevile  alimshambulia Bernie Sanders kwa kumuachia nafasi Bi Clinton kwa kusema kuwa Sanders alifanya makubaliano na ‘shetani’ .

 Hata hivyo wakati wagombea hao kwa nyakati tofauti wakiendelea na kampeni zao baadhi ya  wanachama wa Democrat na Republican wememkosoa Trump kutokana na matamshi yake ambayo amekuwa akiyatoa kila mara dhidi wa wapinzani wake ndani na nje ya chama chake.

Hata hivyo, wachumbuzi wa masuala ya siasa za Marekani wanasema kampeni za Trump zinatoa changamoto kubwa kwa uongozi wa chama cha Republican ambao unaonekana kutompenda kuwa mgombea wake.

  Wanamuona Trump kama “mnoko” na “mchafuzi” wa nafasi ya chama hicho kushinda dhidi ya wapinzani wao wa Democrat. Uongozi wa Republican ungependelea kusimamisha wagombea wengine wasio na utata mkubwa kama Jeb Bush, Marco Rubio, John Kasich au Scott Walker.

 Tayari Trump amezusha mitafaruku mikubwa na misuguano ndani ya nje ya chama kutokana na matamshi yake hasi dhidi ya wahamiaji wenye asili ya Kihispania (hususani kutoka Mexico) ambao alinukuliwa akiwaita wahalifu, majambazi, wauaji na wabakaji.

 Pia amekwaruzana na baadhi ya wanasiasa waandamizi wa chama hicho akiwemo Seneta John McCain na Graham Lindsey ambapo  katika mdahalo wa kwanza ukiwapambanisha wagombea kumi kwenye ulingo mmoja, Trump alisakamwa vikali na wagombea wengine huku akitupiwa maswali magumu na muongozaji wa mdahalo huo, ambayo yasemekana yalilenga kumkata makali.

 Trump alijibu mapigo na kumtupia madongo mazito mwongozaji wa mdahalo huo, Megyn Kelly wa kituo cha Televisheni cha Fox ambacho kina uhusiano wa karibu na viongozi wakuu wa Chama cha Republican.

  Hivi karibuni pia amekwaruza na mgombea binafsi  wa kike Carly Fiorina, ambaye aliwahi kuwa mkuu wa kampuni ya kubwa ya kompyuta ya Hewlett-Packard.

  Tatizo kubwa la Chama cha Republican ni kwamba ingawa hawampendi Trump, ni lazima wawe makini jinsi ya kumkabili, kwa vile mpaka sasa anaonyesha kupendwa na wanachama na watu wengi wa kawaida ambao wamechoshwa na uongo wa “wanasiasa wa ndani”  wa Jiji la Washington.

 Kwa watu wa kawaida, Trump anaonekana kama mgombea tofauti anayesema kitu kutoka moyoni mwake, ambaye anasema ukweli hata kama unauma. Wanamuona Trump kama mtu ambaye ana pesa zake, lakini anataka kusaidia watu wengine kwa dhati na hasukumwi kuwania kiti cha Urais kutokana na “njaa” zake au maslahi binafsi.

 Trump amekuwa akitishia kwamba endapo viongozi wa Chama cha Republican watamchezea mchezo wa rafu, atajitoa chama hicho na kusimama kama mgombea binafsi, hatua ambayo itakiweka chama cha Republican kwenye hali mbaya ya ushindani na mahasimu wao wa chama cha Democrat.

 Wakati hali ikiwa hivyo kwa upande wa Trump hali ni tofauti kwa upande wa hasimu wake mkubwa toka Chama cha Democrat kwani mgombea wake, Hillary Clinton ameendelea kupata uungwaji mkono ndani na nje ya chama chake.

 Kwa mfano mapema wiki hii, Richard Hanna kutoka mjini New York amekuwa mmoja kati ya wanachama wengi kutoka Chama cha Republican waliotamka hadharani kuwa watampigia kura mgombea urais kupitia Democrat, Hillary Clinton.

 Hanna amemwita Donald Trump aibu ya taifa. Wanachama wengine kutoka chama cha Republican wamejitenga kutomshabikia Trump au kumuunga mkono, hali inayozidi kumuweka katika wakati mgumu kuelekea katika uchaguzi Novemba, mwaka huu.

 Kauli za Donald Trump, sera zake dhidi ya wanawake, masuala ya wahamiaji wasiokuwa na nyaraka zinazotakiwa na kuwa akichaguliwa Waislamu hawataingia Marekani, zimewafanya wafuasi wa Republican kusema heri shetani unjuaye, kuliko Malaika usiyemfahamu.

 Katika hatua nyingine Rais wa Marekani, Barack Obama amemshambulia mgombea huyo wa nafasi ya urais kwa tiketi ya Chama cha Republican, Donald Trump, kwa madai ya kutokuwa na sifa stahiki za kuwa Rais wa Marekani.

Obama hakuishia hapo bali amewashangaa wafuasi wa chama cha Republican kwa nini wanendelea kumuunga mkono mgombea huyo Trump ambaye amekuwa tofauti na wagombea waliopita wa Chama cha Republican.

 Pia Rais Obama amemuonya Trump kuwa kadri wanavyoelekea katika uchaguzi, anapaswa kuidhihirishia nchi kuwa akipewa siri za taifa hilo hatazivujisha kwani mdomo wake unaonekana kutokuwa na breki.

Katika hatua nyingine, ukiacha ukweli kwamba Wamarekani wanamwona Trump kama silaha ya migawanyiko ndani ya taifa hilo, hofu imewatawala kutokana na msimamo wake kuwa akiwa Rais wa Marekani atahakikisha anaitawala upya Afrika kwa kuiweka chini ya ukoloni wa Marekani.

Si hilo tu, Bara la Asia, analitaja kama mtambo wa kuzalisha magaidi, hivyo anasema akishika dola atahakikisha analisambaratisha kwa nia ya kurejesha nidhamu na kuifanya Marekani iwe taifa kubwa tena duniani, akidai kwa sasa limepoteza mwelekeo.

Uamuzi wa Trump kuampongeza Waziri wa sasa wa Mambo ya Nje wa Uingereza, Boris Johnson kufanikisha Uingereza kujiondoa katika Jumuiya ya Ulaya (EU) unawafanya Wamarekani waone kuwa Trump akiingia madarakani, kuna hatari ya kuigawa dunia katika vipande isivyostahili.

Wengi wanashauri Trump adhibitiwe, kwani kauli na matendo yake yana hatari ya kuzusha vita kuu ya tatu ya dunia. Kubwa wanalosema ni kwamba Trump ana uelewa finyu wa masuala ya kimataifa na anadhani Marekani ina nguvu za kijeshi kuliko dunia yote ikiwa imeungana.

Wanafafanua kuwa kwa sasa kutokana na deni kubwa linaloikabili Marekani, nguvu ya kiuchumi na kijeshi ziliyonayo nchi kama China na Urusi, zikiungana, jambo ambalo linatarajiwa, Marekani inaweza kupata pigo la mwaka.

Wanaona jaribio la Trump kuchokoza dunia kuwa ni sawa na kuiangusha dola ya Marekani sawa ilivyoanguka dola ya Warumi, ambao walikaa kwenye sherehe na kusahau kuwa vijakazi wana nguvu ya kuwaondoa madarakani wafalme.

Trump ameanza kulalamika kuwa kuna hatari ya kura zake kuibwa, suala lililowafanya Wamarekani kumuona kama mfa maji, baada ya kubaini kuwa sera zake hazikubaliki. Mwanasiasa huyo, hajawahi kuwa ndani ya chombo chochote cha kisiasa, bali ana uwezo mkubwa wa kifedha kutokana na biashara ya kujenga na kuuza nyumba katika sehemu mbalimbali duniani. 

Wakati vita vya maneno katika kampeni hizo vikipamba moto, Mkuu wa Kamati Kuu ya Chama cha Democrat, nchini Marekani, Amy Dacey amejiuzulu nafasi hiyo. Uamuzi huo wa kujiuzulu umetokana na kuvuja kwa maelfu ya barua pepe zenye kuonesha mapendekezo ya Chama cha Democrat zenye kuandaa njama za makusudi kudhoofisha kampeni ya Hillary Clinton dhidi ya mpinzani wake wa zamani, Bernie Sanders aliyekuwa mgombea urais.

 Dacey kuachia kwake ngazi anakuwa mtu wa pili kujiuzulu baada ya Mwenyekiti wa wanawake wa chama hicho, Debbie Wasserman Schultz kujiuzulu kabla ya Mkutano Mkuu wa Taifa wa Chama cha Democrat mjini Philadelphia wiki iliyopita, kutokana na kashfa hiyo.

 Novemba 8, 2016 Wamarekani watapiga kura za majimbo (electoral college) kuchagua wachaguzi (electors) ambao kwa niaya ya kura za wananchi (popular votes) hufanya kazi ya kuchagua Rais na Makamu wa Rais wa chama husika.

 Kwa mujibu wa sheria, mgombea urais anayeshinda kura za wananchi katika Jimbo lolote kati ya majimbo 50, huchukua kura zote za jimbo hilo, na wajumbe wanaowakilisha jimbo katika mkutano wa kitaifa wa kumchagua Rais na Makamu wake, hawana hiyari ya kuchagua mgombea mwingine, isipokuwa aliyeshinda katika kura za wananchi (popular vote).

 Mbali na kura hizo za majimbo 50, Wilaya ya Colombia au maarufu kama Washington DC, pia inazo kura tatu za majimbo ambazo nazo huchukuliwa na mtu aliyepata ushindi wa jumla katika kura za wananchi.

 Hata hivyo, majimbo mawili ya Maine na Nebraska ndiyo pekee ambayo wajumbe wake wanaochaguliwa kupiga kura za kumchagua Rais hawabanwi kumpigia aliyeshinda kura ya Jimbo.

Kwa maana rahisi, ni kwamba Wamarekani hawamchagui Rais wao moja kwa moja, isipokuwa kupitia wawakilishi wanaochaguliwa siku ya uchaguzi kwa kushinda kura katika jimbo husika.

Mfano katika uchaguzi wa Novemba 6, mwaka 2012, Rais Barack Obama alipata kura za majimbo 332, akashinda katika majimbo 26 na Wilaya ya Colombia (Washington D.C), huku mpinzani wake Mitt Romney kutoka chama cha Republican akishinda katika majimbo 24 pekee na kupata kura za majimbo 206. Mshindi alihitaji kupata kura za majimbo 270.

Katika kura za wananchi (popular vote) Obama alipata kura 65,915,796 sawa na asilimia 51.1 na mpinzani wake mkuu, Romney akapata kura 60,933,500 sawa na asilimia 47.2.

Kwa Marekani mgombea anayepata kura nyingi za wananchi si lazima ndiye awe mshindi. Mshindi anapatikana kwa wingi wa kura za majimbo (electoral college), ambazo kura hizi nazo zinatokana na wingi wa watu kwa kila jimbo. Kila watu 30,000 kwa Marekani wanawakilishwa na mbunge mmoja. Uchaguzi wa Novemba 7, 2000, aliyekuwa mgombea wa Democrat, Al Gore alishinda kura za wananchi kwa kupata kura za wananchi (popular vote) 50,999,897 sawa na asilimia 48.4, dhidi ya kura za mgombea wa Republican George W. Bush aliyepata kura 50,456,002 sawa na asilimia 47.9, lakini Gore hakuwa Rais wa Marekani.

Kilichotokea, Bush alishinda kura za majimbo 271, zikiwamo kura 55 za Jimbo la California, ambalo lilikuwa linaongozwa na mdogo wake, Jeb Bush. Jimbo hili lilibishaniwa mahakamani hadi Januari 20, mwaka 2001, na ilipofika saa 6 mchana, kwa mujibu wa Katiba ya Marekani, kesi zote za uchaguzi wa kupinga matokeo ya urais hujifuta ikiwa hazijatolewa uamuzi na hata kama Rais aliyetangazwa na Tume anakuwa hajaapishwa, ikifika muda huo hupewa ulinzi rasmi na kuchukuliwa kuwa Rais mtangulizi wake ameondoka marakani na Rais Mteule (president elect) amechukua nchi.

Katika kinyang’anyilo hicho, Bush alishinda kura 271 za majimbo, ikiwa ni kura moja zaidi ya kura zilizohitajika yaamini 270 kupata urais wa Marekani. Gore alipata kura za majimbo 266, na akashinda majimbo 20 na Wilaya ya Colombia (Washington DC), huku Bush akishinda majimbo 30 yaliyompa kura za majimbo nyingi kuliko mpinzani kwake.

Uchaguzi wa mwaka 2000 uliacha historia ya pekee kati ya chaguzi 57 zilizopita kwa kuwachagua marais 44 wa nchi hiyo, ambapo kwa mara ya kwanza kura za Gore ziliibwa wazi kwa utaratibu ambao mashine za kupigia kura kwa Gore zilikuwa zimetengenezwa kiteknolojia kiasi kwamba mtu aliyempigia Gore kura ilikuwa haionekani, na aliyempigia Bush ilionekana vizuri mno.

Kutokana na mtafaruku huo, Wamarekani walilazimika kuhesabu kura za California kwa mikono kwa zaidi ya mwezi mzima, lakini kama makala hii inavyoeleza hapo juu ilipofika Januari 20, 2001, kesi zote zilijifuta mahakamani na Bush akatangazwa kuwa Rais wa Marekani. Hofu hiyo ndiyo inampata Trump kuwa sawa na Bush alivyodaiwa kuiba kura mwaka 2000, kuna uwezekano mkubwa mwaka huu kura zake zikaibwa kwani wakubwa wengi hawampendi.

Novemba 8, mwaka huu Hillary Clinton na Donald Trump wataingia ulingoni kutafuta kura za majimbo 270. Hadi kufikia mwishoni mwa wiki, utabiri ulikuwa ukionyesha Clinton akiongoza kwa kura na kura za majimbo 217, dhidi ya kura 291 za Trum. Clinton anaendelea na kampeni kuwafikia wapigakura za majimbo 53 ambao hadi sasa hawajaamua wampigie nani, ikilinganishwa na Trump anayetafuta 79 kufikisha idadi ya 270 kushinda urais. Hata hivyo, kura za majimbo za Trump zina mwelekeo wa kushuka siku hadi siku kutokana na kauli zake tata dhidi ya Wamarekani wenzake na dunia kwa ujumla.

Pigo kubwa alilonalo Trum, ni kuwa marais wote watano wa Marekani wanaoishi kwa sasa, George H. W. Bush (Republican), Barack Obama (Democrat), George W. Bush (Republican), Bill Clinton (Democrat), and Jimmy Carter (Democrat). wanampinga bila kujali vyama vyao, wampinga wakisema hafai kuwa Rais wa Marekani kutokana na matendo na kauli zake bila kujali itikadi za vyama vyao.

By Jamhuri