Katika historia, Tanzania hakijatokea kipindi ambacho udini umepewa nafasi kubwa ya kuvuruga amani ya Tanzania kama kipindi hiki.

Lakini pia hakijatokea kipindi ambacho si kama tu maisha ya viongozi wa makanisa yametishiwa, bali pia mpango wa kuwaua viongozi hao unatekelezwa.

 

Yote haya ni matokeo ya Serikali kumwacha huru bila kumchukulia hatua yeyote mtu anayesambaza CD za kuhamasisha Waislamu wawaue viongozi wa makanisa. Hii ni kusema kwamba tumeruhusu mauaji ya viongozi wa makanisa.

 

Katikati ya vitisho hivyo na mauaji ya viongozi wa makanisa, inashangaza, tena inatisha kusikia kwamba eti viongozi wa polisi hawajui kama kuna vitisho dhidi ya viongozi wa makanisa.

 

Habari za CD ya video inayohamasisha mauaji ya viongozi wa makanisa sisi sote tumezipata siku nyingi. Sasa kama viongozi wa polisi wanaodai kuwa wao ndiyo usalama wa raia wanasema kwamba hawana habari za CD kama hiyo, basi hapa hakuna usalama wa raia, hasa wa viongozi wa makanisa na wafuasi wao.

 

Tulianza na kusoma katika gazeti la Kikristo la kila wiki toleo la Januari mwaka huu, kwamba Waislamu wanahamasishana kumuua Policarp Kardinali Pengo. Gazeti lilieleza waziwazi kwamba sheikh mmoja wa jijini Mwanza, amekuwa akisambaza DVD zinazowahamasisha Waislamu nchini na Afrika Mashariki kwa ujumla, kuwaua Wakristo wakiwamo viongozi wao wa dini.

 

Sheikh huyo wa jijini Mwanza anadai katika DVD hizo kuwa kuanzia sasa Waislamu wanapaswa kuachana na jihad ya maneno matupu, na badala yake watumie bunduki za kivita kupambana na Wakristo na viongozi wao.

 

Wakati ule Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam aliliambia gazeti lile la Kikristo kuwa wanakusanya taarifa zaidi kuhusiana na kusambazwa kwa DVD hizo ili wachukue hatua. Hadi leo polisi haijachukua hatua yoyote, kwa vyovyote hatua ya kwanza ingekuwa kukamatwa kwa sheikh huyo wa jijini Mwanza, lakini hajakamatwa huku Waislamu wakiwa wameanza kutekeleza mauaji ya viongozi wa makanisa ambayo yeye amehamasisha!


Wakati gazeti lile la Kikristo lilisema kwamba DVD inahamasisha auawe Kardinali Pengo, gazeti jingine la kila wiki limesema kwamba sasa Waislamu wanahamasishwa kuwaua viongozi wengine wa makanisa mbali ya Kardinali Pengo.

 

Hakijatokea kipindi chochote katika historia ya Tanzania, ambacho viongozi wa makanisa na wafuasi wao wanaishi katika hali ya wasiwasi kama kipindi hiki. Wote wako roho juu!

 

Ni katika mazingira hayo mwishoni mwa mwaka jana Jukawaa la Wakristo (TCR) lilikaa na kutafakari nchi ilipofikishwa. Kikao hicho kilijumuisha viongozi 37 wa makanisa kutoka Kanisa Katoliki, Jumuiya ya Kikristo (CCT), na Baraza la Makanisa ya Kipentekoste ya Tanzania (PCT).


Katika tamko lao, viongozi hao wa makanisa walieleza kwamba zipo mbinu chafu ambazo zimekuwa zikifanywa na baadhi ya waumini wa dini ya Kiislamu, kwa kutumia vyombo vya habari vya dini kukashifu Ukristo, pamoja na kukaa vikao mbalimbali kwa lengo la kuwaua wachungaji na maaskofu.

 

Tamko lilisema pia kwamba kitendo cha Serikali ya Rais Kikwete kukaa kimya wakati vitisho dhidi ya maisha ya viongozi wa makanisa vinapamba moto, kinaleta picha kwamba Serikali inakubaliana na kashfa, hujuma za kuchoma makanisa na mali za makanisa.

 

Kwa vyovyote, kama Serikali isingekubaliana na vitendo hivyo viovu, ingemkamata siku nyingi mtu anayehamasisha mauaji hayo – sheikh huyo wa jijini Mwanza – ambaye inasemekana kwamba si raia wa Tanzania. Kwanini serikali inamwacha sheikh huyo kuvuruga amani bila kumkamata? Kwa vyovyote Wakristo wanalo jibu.


Kwa bahati nzuri viongozi wa makanisa walitaka kukutana na Rais Kikwete ili kujadiliana naye kuhusu hali halisi inavyoendelea nchini. Lakini Ikulu iliwapuuza. Hili ni jambo la hatari sana maana tunachojua ni kwamba mtu hakatai kuitwa bali hukataa aitiwalo.

 

Huko nyuma wakati maovu hayo yalipokuwa yakitokea Zanzibar, ilidaiwa kuwa lengo lilikuwa kuukataa Muungano ili wa Bara walioko Zanzibar warudi kwao Bara. Sasa hata viongozi wa makanisa walioko Bara wanataka kuuawa. Maana yake ni nini?

 

Hapana shaka lengo ni kuufuta Ukristo Tanzania. Wakristo wanajua hilo. Ni katika mazingira haya sasa kuna habari kwamba Wakristo wanahamasishana kutomchagua Mwislamu kuwa rais mwaka 2015. Kwao imetosha.

By Jamhuri