Urusi imeionya Uingereza kutokana na kitendo chake cha kuwafukuza wanadiplomasia wake
23, baada ya kuituhumu nchi hiyo kuhusika na shambulizi la sumu dhidi ya jasusi wa zamani wa
Urusi aliyekuwa akiishi uhamishoni Uingereza.
Kufukuzwa kwa raia hao wa Urusi, kulitokana na madai ya nchi hiyo kuituhumu Urusi
kuhusika na shambulizi la sumu dhidi ya jasusi Sergei Skripal na binti yake Yulia, katika mji wa
Salisbury nchini Uingereza.
Waziri Mkuu wa Uingereza, Theresa May, siku za karibuni aliwapa wiki moja ya kuondoka raia
23 wa Urusi ambao alisema walikuwa majasusi waliofanya majukumu yao chini ya mwavuli wa
diplomasia.
Wakati serikali ya Urusi ikitoa lawama hizo kwa Uingereza, taarifa ya pamoja iliyotolewa na nchi
za Uingereza, Marekani, Ufaransa na Ujerumani imelaani shambulizi hilo la sumu dhidi ya
jasusi huyo wa zamani wa Urusi.
Taarifa hiyo imeitaka serikali ya Urusi kutoa taarifa kamili ya mpango wa sumu aina ya
Novichok kwa shirika la kudhibiti silaha za sumu bila ya kuchelewa kuliko kuanza kutoa vitisho
vya kujihami dhidi ya tukio hilo.
Jasusi huyo pamoja na binti yake bado wanaelezwa kuwa katika hali mbaya hospitalini, tangu
walipobainika kuathiriwa na sumu tangu Machi 4 mwaka huu, huku wakisemekana kuwa katika
hali mbaya.
Hata hivyo, serikali ya Urusi kwa kupitia Waziri wake wa Mambo ya Nje, Sergei Lavrov,
imekana kuhusika kwa namna yoyote na tukio hilo kiasi cha kuitaka Uingereza kuomba radhi
juu ya shutuma hiyo.
Lavrov amesema nchi yake inatarajia kujibu mapigo siku za karibuni dhidi ya hatua ya
Uingereza kuwafukuza raia wake, na kuongeza kuwa maafisa wa Uingereza nchini
humo watajulishwa juu ya hatua zitakazochukuliwa siku chache zijazo.
Msemaji wa Ikulu ya Urusi – Kremlin Peskov, kwenye mkutano wake na waandishi wa habari
kwa njia ya simu amenukuliwa akisema kuna dalili za uchokozi dhidi ya taifa hilo, na kusisitiza
kuwa Urusi haihusiki na tukio hilo.
Nae Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron, amesema anaunga mkono tathmini ya Uingereza
kuwa Urusi ndiyo iliyohusika na shambulizi dhidi ya jasusi huyo na kuapa kuchukua hatua ya
kuhusiana na shambulizi hilo.

By Jamhuri