Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam, Kisutu, imetoa amri ya zuio la mali za Mhasibu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Godfrey Gugai.
Amri ya Mahakama ya Kisutu ilitolewa Mei 8, mwaka huu; na Gugai anatarajiwa kufikishwa mahakamani kujibu mashitaka ya rushwa na mengine kulingana na tuhuma zinazomkabili.
Kuzuiwa kwa mali hizo kumetokana na maombi yaliyowasilishwa mahakamani na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) chini ya kifungu namba 38(1)(a) na (b) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Namba 11 ya mwaka 2007 katika shauri Namba 13 la mwaka 2017.
Mahakama ya Kisutu imeamuru yafuatayo kuhusu mali hizo:
1: Mali zote (zilizoorodheshwa hapa) ziwe chini  ya zuio la Mahakama.
2: Gugai, mawakala wake na watu wengine wote wanaomwakilisha wanazuiwa kuuza au kuhamisha umiliki au kuweka dhamana mali zote zilizowekewa zuio.
3: Msajili wa Hati ameagizwa kusajili zuio hilo kama kizuizi dhidi ya mali zote zilizotajwa.
4: Msajili Msaidizi wa magari ameagizwa asiruhusu uhamishaji wa umiliki wa vyombo vya usafiri vilivyowekewa zuio.
Takukuru kwa upande wake imesema: “Tunawaomba wananchi na umma kwa jumla kuzingatia zuio hili la Mahakama dhidi ya mali za Bwana Godfrey Gugai na kutojihusisha na biashara ya aina yoyote ile kuhusiana na mali hizi na hatutawajibika kwa madhara yoyote yanayotokana na kujihusisha na mali hizi.”

Msimamo wa Rais Magufuli
kuhusu rushwa na ufisadi

 
Rais John Magufuli, akizindua Bunge mnamo Novemba 20, 2015; pamoja na mambo mengine, alizungumzia msimamo wa Serikali yake katika mapambano dhidi ya rushwa. Alisema:
“Jambo moja nililolisemea kwa nguvu kubwa wakati wa kampeni ni mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi. Sikufanya hivyo kwa sababu nilitaka tu kuwarubuni wananchi ili wanipe kura zao na kunifanya kuwa Rais wao. Nililiongea jambo hili kwa dhati kabisa, na nilichokisema na kuwaahidi wananchi ndicho hasa nilichokikusudia.
“Wananchi wanachukia sana rushwa na ufisadi, na wamechoshwa na vitendo hivyo. Mimi pia ninachukia rushwa na ufisadi. Sifurahishwi kabisa na vitendo vya rushwa na ufisadi vinavyoendelea hapa nchini. Vitendo vya rushwa na ufisadi vinawanyima haki wananchi na kuitia hasara serikali kwa mamilioni ya fedha ambazo zingeweza kutumika kwa ajili ya kujenga miradi ya maendeleo kwa ajili ya watu wetu.


“Chama changu, Chama Cha Mapinduzi, kimejengwa katika misingi ya kukataa rushwa na ufisadi. Ndio maana moja ya Imani kuu za CCM ni ile isemayo: ‘Rushwa ni adui wa haki, sitatoa wala kupokea rushwa’.
“Kwa Mtanzania mwaminifu kwa imani yake hatakuwa na kigugumizi katika kuwa mstari wa mbele katika kupambana na rushwa na ufisadi.
“Mmoja wa waasisi wa Taifa letu, Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliwahi kuifananisha rushwa na ufisadi ‘Kama Adui Mkubwa wa Watu’. Akiongea Bungeni Mei 1960, Mwalimu Nyerere alisema yafuatayo kuhusu rushwa:
‘Rushwa [na ufisadi] havina budi kushughulikiwa bila huruma kwa sababu naamini wakati wa Amani rushwa na ufisadi ni adui mkubwa kwa ustawi wa watu kuliko vita.’
“Haya ni maneno makali ya mtu na kiongozi aliyeichukia na kuikemea rushwa katika maisha yake yote ya uongozi. Ni maneno yanayotukumbusha tu nini kinaweza kikatutokea kama taifa endapo tutaendekeza rushwa na ufisadi. Chuki za wananchi dhidi ya rushwa na ufisadi ni dhahiri, wamechoka kabisa, wamechoka sana, hawako tayari kuvumilia upuuzi wa serikali itayoonea haya rushwa na kulea mafisadi.


“Mimi nimewaahidi wananchi, na nataka niirejee ahadi yangu kwao mbele ya Bunge lako tukufu, kwamba nitapambana na rushwa na ufisadi bila kigugumizi na bila haya yoyote. Dawa ya jipu ni kulitumbua, na mimi nimejipa kazi ya kuwa mtumbua jipu. Najua kutumbua jipu kuna maumivu lakini bahati mbaya halina dawa nyingine. Hivyo ninaomba Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote mniombee na muniunge mkono wakati natumbua majipu haya.
“Ninafahamu ugumu wa vita niliyoamua kuipigana. Nasema nafahamu ugumu na changamoto zake kwa sababu wanaojihusisha na rushwa sio watu wadogo wadogo. Vitendo vya rushwa na ufisadi vyenye madhara makubwa kwa nchi na ustawi wa nchi yetu hutendwa na watu wenye dhamana kubwa za uongozi na utumishi ambazo wamezipata kutokana na ridhaa ya watu. Kwa hivyo ili niweze kufanikiwa lazima nipate ushirikiano mkubwa toka kwa Bunge lako tukufu na vyombo vingine vilivyopo na vyenye majukumu ya kupambana na vitendo hivi.
“Aidha, tutashinda vita hii endapo wananchi pia watatuunga mkono. Sina mashaka kuwa kwa vile wao, kwa wingi wao, wanachukia rushwa na ufisadi, watakuwa tayari kutoa ushirikiano wao katika mapambano haya dhidi ya rushwa na ufisadi.
“Katika kushugulikia tatizo hili nimeahidi kuunda Mahakama ya Rushwa na Ufisadi. Ni matumaini yangu vyombo husika katika jambo hili havitanikwamisha.


“Aidha, nataka niahidi mbele ya Bunge lako tukufu kwamba, kiongozi yeyote wa kuteuliwa, ambaye mimi nitakuwa nimemteua kwa mamlaka niliyonayo kikatiba, na ninayo mamlaka ya kumwajibisha, pindi tu nikibaini na kujiridhisha kuwa anajihusisha na vitendo vya rushwa na ufisadi nitamtimua mara moja. Baada ya mimi kuchukua hatua hizo hatua na taratibu zingine za kisheria zitafuata.
“Ninachotaka kusema ni kuwa Serikali yangu itafuatilia kwa karibu mienendo ya viongozi na watendaji wake ili kubaini kwa haraka nani anajihusisha na vitendo vya rushwa na ufisadi. Na tukishajiridhisha hatutasubiri, tutachukua hatua. Ni imani yangu wengine pia katika ngazi mbalimbali mtafanya hivyo. Kwa sababu bila kufanya hivyo rushwa na ufisadi vitazoeleka na kuwa wimbo unaoburudisha badala ya kuudhi na kukera.”

MALI ZA GUGAI

1: Nyumba nne za ghorofa moja zilizoko kiwanja na. 64 kitalu B, Ununio, Kinondoni

2: Nyumba tatu za ghorofa moja zilizoko kiwanja na.150 kitalu 8, Bunju, Kinondoni

3: Nyumba zilizoko kwenye kiwanja na. 225 kitalu 6, Mbweni JKT, Kinondoni

4: Nyumba zilizoko kwenye kiwanja na. 62 na 63 kitalu C, Kinondoni

5: Nyumba iliyoko kiwanja na. 29 kitalu L, Majita, Musoma

6: Nyumba namba 713 PPF Kiseke Mwanza

7: Nyumba iliyoko kiwanja na. 438 kitalu D, Nyegezi, Mwanza

8: Kiwanja na. 14 kitalu J, Bunju, Kinondoni

9: Kiwanja na. 47 Kitalu B, Mwongozo, Kigamboni

10: Kiwanja na. 184 Kitalu B, Buyuni, Temeke

11: Kiwanja na. 103 Kitalu L, Kaole, Bagamoyo

12: Kiwanja na. 104 Kitalu L, Kaole, Bagamoyo

13: Kiwanja na. 209 Kitalu B, Kibaha

14: Kiwanja na. 195 Kitalu 3, Kihonda Morogoro

15: Kiwanja na. 993 Kitalu L, Kiegeya, Morogoro

16: Kiwanja na. 868 Kitalu Q, Lukobe Morogoro

17: Kiwanja na. 34 Kitalu K, Kisasa B, Dodoma

18: Kiwanja na. 32 Kitalu N, Itega, Dodoma

19: Kiwanja na. 39 Kitalu M, Itega, Dodoma

20: Kiwanja na. 24 Kitalu B, Chidachi, Dodoma

21: Kiwanja na. 64, Nzuguni, Dodoma

22: Kiwanja na.  230 Kitalu B, Nyegezi, Mwanza

23: Kiwanja na. 439, Kitalu D, Nyegezi, Mwanza

24: Kiwanja na 275 Kitalu 2, Nyamhongolo, Mwanza

25: Kiwanja na. 277 Kitalu 2, Nyamhongolo, Mwanza

26: Kiwanja na. 296 Kitalu 2, Nyamhongolo, Mwanza

27: Kiwanja na. 297 Kitalu 2, Nyamhongolo, Mwanza

28: Kiwanja na. 286 Kitalu G, Nyamagana, Mwanza

29: Kiwanja na. 287 Kitalu G, Nyamagana, Mwanza

30: Kiwanja na. 90 kitalu 5, Bugarika, Mwanza

31: Kiwanja na. 126 KItalu A, Makoko, Musoma

32: Kiwanja na. 621 na 623 Kitalu A, Gomba, Arusha

33: Kiwanja na. 622 Kitalu A, Gomba, Arusha

34: Kiwanja na. 737 Kitalu C, Mwambani, Tanga

35: Kiwanja na. 1, 2 na 3 Kitalu J, Mwambani, Tanga

36: Kiwanja na. 4 Kitalu J, Mwambani, Tanga

37: Kiwanja na. 5 Kitalu J, Mwambani, Tanga

38: Kiwanja na. 18 Kitalu J, Mwambani, Tanga

39: Kiwanja na. 79 Kitalu J, Mwakidila, Tanga

40: Kiwanja na. 1113 Kitalu J, Mwakidila, Tanga

41: Gari na,na T 180 DBQ, Mitsubish Canter

42: Gari namba T 581 BQU, Toyota Hillux

43: Gari namba T 814 CSC, Nissan Murrano

44: Gari namba T 679 ASD, Toyota RAV 4

45: Gari namba T 913 DHE Suzuki

46: Pikipiki namba MC 837 BCL

By Jamhuri