Vigogo wa Kampuni ya Six Telecoms Waendelea Kusota Rumande

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imetaja tarehe nyingine ya kuendelea na kesi ya uhujumu uchumi na kusababisha hasara ya USD 3.7 milioni ambayo ni sawa na bilioni nane inayowakabili vigogo wanne wa Kampuni ya Six Telecoms Limited na kampuni yenyewe.

Hatua hiyo imekuja baada ya wakili wa upande wamashitaka, Jackline Nyantori kuieleza mahakama kuwa, upelelezi dhidi ya kesi hiyo bado haujakamilika na wanajitahidi kukamilisha mapema iwezekanavyo.

Watuhumiwa katika kesi hiyo ni Mhandisi na Mkurugenzi Mkuu wa kampuni ya Six telecoms, Hafidhi Shamte, Mfanyabiashara na Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Peter Noni, Mwanasheria na Mhadhiri na Mkurugenzi wa hiyo kampuni Dr ,Ringo Tenga, Mkuu wa fedha wa kampuni hiyo Noel Chacha na Kampuni ya Six Telecoms Limited.

Wakili wa utetezi Masumbuko Lamwai akizungumza mahakamani hapo amedai upelelezi wa kesi wanayokabiliwa nayo washtakiwa siyo mpya, kwani ilishafikishwa mahakamani hapo kama kesi ya uhujumu uchumi Namba 2 ya mwaka 2016.

Wakili wa utetezi amedai, upande wa mashtaka wanazo taarifa zote juu ya shauli hilo sababu mashtaka wanayoshtakiwa nayo yanahusu taarifa za simu ambazo ni electronic na ziko recodedi hivyo hamna ushahidi wowote ambao bado haujakamilika.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Desemba 15 mwaka huu, washtakiwa wamerudishwa rumande.