Rais wa Urusi Vladimir Putin ametangaza kuwa atawania kiti cha urais kwa mara nyingine tena katika uchaguzi mkuu wa mwaka ujao wa 2018.

Alitangaza hayo alipokuwa akiwahutubia wafanyikazi huko Nizhny Nov-gorod.
Rais Putin ambaye ana umri wa miaka 65 alichaguliwa kwa mara ya kwanza kuwa Rais wa Urusi mwaka 2000.
Baada ya kuhudumu kwa mihula miwili alichaguliwa kama Waziri mkuu na mrithi wake Dmitry Medvedev kwa muhula mmoja.

Alichaguliwa tena kama rais mwaka 2012 baada ya muhula wa Rais kuongezwa kutoka miaka minne hadi sita.
Kura ya maoni inaonesha kuwa Putin, ataibuka mshindi katika uchaguzi huo mkuu utakaofanyika mwezi Machi mwakani na akishinda basi ataongoza taifa hilo hadi 2024.

Mwanahabari wa runinga Ksenia Sobchak ni miongoni mwa waliotangaza kwamba watawania kwenye uchaguzi huo.
Kiongozi mkuu wa upinzani Alexei Navalny hawezi kuwania baada ya kupatikana na makosa ya ufujaji wa fedha za umma, mashtaka ambayo anasema yalichochewa na siasa.

By Jamhuri