Walioshtakiwa ulaji rushwa Kenya kukaa rumande wiki moja

Watuhumiwa 24 walioshtakiwa kuhusiana na kashfa ya ufujaji wa pesa katika Shirika la Vijana wa huduma kwa Taifa (NYS) watakaa rumande kwa wiki moja.

Jaji ameamuru wazuiliwe hadi Jumatano wiki ijayo ambapo uamuzi wa kuachiliwa kwa dahamana utatolewa.

Miongoni mwa walioshtakiwa jana ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Vijana na Jinsia Lilian Mbogo Omollo na Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo Richard Ndubai.

Walikamatwa na wengine wakajisalimisha kwa polisi Jumatatu wiki hii na kisha kufikishwa kortini Milimani, Nairobi jana.

Kikao cha kusikizwa kwa kesi dhidi yao kiliendelea hadi usiku wa manane.