Wanaume watelekeza watoto walemavu Arumeru

*Wanawake wasukumiwa mzigo

Tatizo la wanaume kuwatelekeza watoto wao wenye ulemavu, limetajwa kukithiri katika Kijiji cha Ambureni, Wilaya ya Arumeru, mkoani Arusha.

Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na JAMHURI hivi karibuni, umebaini kuwapo kwa familia zaidi ya 15 zenye watoto walemavu zilizotelekezwa na waume, hivyo wanawake kuachiwa mzigo wa kuzilea.

 

Tabia hiyo imesababisha familia hizo kuishi katika mazingira magumu ikiwa ni pamoja na kuishi katika nyumba za kupanga, huku zikiwa hazina kazi za kujipatia kipato.  Mateso yanayowakabili wanawake hao yanatokana na kujifungua watoto wenye ulemavu, kwani bila kujifungua watoto hao wangeendelea kuishi na waume zao.

 

Zeana Athuman, mkazi wa Ambureni ambaye pia ni mwanawake aliyeathirika na hali hiyo, anasema mume wake aliondoka nyumbani baada ya kujifungua mtoto mwenye ulemavu.

 

“Baada ya kujifungua mume wangu alitoroka nyumbani na akaniacha nikiwa peke yangu katika hali ngumu kimaisha,” anasema Zeana.

 

Alijifungua mtoto mwenye ulemavu wa kutoona, kutotembea, kutosikia na kutozungumza.

 

“Mume wangu alimwona mwanangu kama mkosi ndani ya familia, alinikimbia mtoto akiwa na mwezi mmoja,” anasema.

 

Anaongeza kwamba tangu mumewe amkimbie ni miaka 11 imepita sasa, jambo linaloendelea kufanya maisha yake na mtoto wake kuwa magumu zaidi.

 

Zeana anasema ili kukidhi mahitaji yake na mtoto wake kwa siku, analazimika kumuacha mwanaye huyo kwa majirani aweze kutafuta fedha za kujikimu. Changamoto iliyopo ni kwamba muda mwingi mtoto huyo hufungiwa ndani wakati wote ambao mama yake hutoka kwenda kutafuta riziki.

 

JAMHURI pia inakutana na mtoto anayetajwa kwa jina moja la Terezia (6) mwenye ulemavu anayeishi na bibi yake. Taarifa zinasema baba mzazi wa mtoto huyu aliondoka nyumbani hapo baada ya kuona mtoto wake ni mlemavu.

 

Wakati baba akiwa amemtoroka mwanaye, mtoto huyu anatajwa kuwa katika mazingira magumu zaidi kwani hata mama yake naye hulazimika kuondoka nyumbani na kumuacha akiwa peke yake.

 

“Mtoto huyu alizaliwa akiwa mzima, baada ya miezi saba hali yake ilianza kubadilika akawa haoni wala kusikia ndipo baba mzazi alipoamua kuondoka nyumbani.

 

“Mama mzazi naye alianza kumficha ndani kwa madai kuwa anaogopa watu kumsema amezaa mtoto mlemavu.

 

“Baada ya majirani kugundua tatizo hilo waliamua kwenda kumtoa ndani kwa nguvu na kuanza kumshindisha nje kama watu wengine,” anasema bibi wa Terezia bila kutaja jina lake.

 

Kutokana na changamoto zinazowakabili wanawake wenye watoto walemavu kijijini hapo, hatimaye wamebuni mbinu za kulea watoto wa watu (yaya) ili wapate kipato cha kuendesha maisha yao.

 

Mwalimu wa kituo cha kulelea watoto wenye ulamavu katika Shule ya Msingi Moivaro wilayani Arumeru, Leah Ndaga, anataja changamoto zinazowakabili katika kazi hiyo.  Mwalimu Leah anasema kwamba kwa muda mrefu sasa wananchi wamekuwa wakibeza aina ya kazi wanayoifanya kwa madai kuwa wanapoteza muda kukaa na watoto wenye ulemavu.

 

“Tunatoa elimu kwa jamii na maeneo yanayotuzunguka kuwa watoto hawa ni sehemu ya jamii yetu. Tunaiomba jamii iwachukulie kama sehemu yao isiwatenge badala yake iwasaidie wanapohitaji msaada ukiwamo wa kwenda shuleni,” anasema.

 

Wakati wakiendelea na juhudi za kusaidia miundombinu ya kwenda eneo moja hadi jingine, kituo hicho kina watoto 47. Kati ya hao, watoto watatu wana ulemavu wa macho huku wengine wakiwa na ulemavu wa kutosikia, kutoongea na kutotembea.

 

Mwenyekiti wa Kitongoji cha Msovero, Sioni Mathayo, akizungumzia changamoto hiyo anasema imekuwa vigumu kuwasaidia watoto hao kutokana na kutokuwa na kipato cha kutosheleza mahitaji.

 

“Serikali ya kitongoji hatuna mafungu ya kusaidia watoto walemavu. Tunaomba viongozi wajaribu kuangalia upya jinsi ya kuziwezesha serikali za vitongoji ambazo zipo na wananchi,’’ anasema Mathayo.

 

Pamoja na kutokuwa na bajeti, Mwenyekiti huyo anabainisha kuwa kama kiongozi alichukua jukumu la kupeleka matatizo hayo kwenye uongozi wa juu ili kupata msaada wa namna ya kuwabana wanaume hao wasizikimbie familia zao.

 

Anasema juhudi nyingine zinazofanywa ni za kuwapatia msaada kupitia Kituo cha Aston Vision kilichopo kijijini hapo, ambacho hutoa elimu kwa watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu.

 

Mwasisi wa kituo hicho, Aston Simoni, anasema lengo la kuanzisha kituo hicho lilitokana na kijiji hicho kuwa na watoto wengi wenye ulemavu na wanaoishi katika mazingira hatarishi.

 

“Hapa tunapata msaada kutoka kwa wadau wa nje na ndani ya nchi ambao hutusaidia chakula, magodoro na dawa za kuongeza vitamini kwa watoto yatima na wale wenye walemavu.