Yah: Tuliangalie sakata la elimu kwa sasa [2]

Wiki jana nilizungumzia juu ya elimu ya kambo wakati nikihitimisha barua yangu. Nilijaribu kuangalia tofauti za elimu ya sasa na ya zamani japokuwa hazipaswi kufananishwa kutokana na mitaala na manufaa baada ya masomo. Sisi tulifundishwa kujitambua na kujitegemea na ninyi kwa sasa mnafundishwa kutegemea na kutojitambua.

Katika barua yangu nilihoji juu ya nidhamu ya mwanafunzi wa sasa na yule wa zamani, niliwaangalia hao dotcom na hayo maendeleo ambayo yanakuja kidotcom zaidi, kwamba sasa badala ya kujua kulima bustani unaweza ukagoogle na kupata taarifa mbalimbali zinazohusu kilimo. Hii ndiyo mitaala mipya ambayo inatungiwa mitihani.

Sina nia mbaya ya kutaka kupingana na elimu ya sasa, lakini hoja yangu ni juu ya malezi yanayowakabili hawa wanafunzi ambao ni wanetu na taifa la kesho. Najua maendeleo yanakuja na changamoto zake, lakini pia changamoto hizo lazima zikabiliane na uhalisia wa maisha.

Sisi wazazi tuna dhima kubwa katika kuilea familia yetu ya sasa ambayo ndiyo taifa la kesho, ikiwamo walimu kufanya kazi yao ya kuwapa elimu na mafunzo mengine ya kidunia, wazazi kwa upande wetu tunatakiwa kujua kuwa watoto wetu wana mipaka ya kuishi nao, kisha baada ya miaka kumi na minane wanakutana na walimwengu ambao ni pamoja na kuwa na familia zao.

Maswali tunayopaswa kujiuliza ni mengi ikiwamo na kujua kama malezi tunayowapa sasa yanakidhi kiwango cha kujitegemea na kuishi na jamii inayowazunguka? Mathalani, nidhamu gani ambayo tunawalea nayo wanetu, tumefika mahali ambapo tunadhani tunatakiwa kuiga malezi ya zamani ama la? Tunaona fahari tunayoyaona kama malezi bora hivi sasa?

Jamii yoyote iliyostaarabika inaangalia  mambo mengi ya msingi, nidhamu ikiwa ni moja ya vigezo vinavyohusika. Nimejaribu kuangalia suala la nidhamu kwa watoto wetu ambao wengi wao ni wanafunzi wa siku hizi, sipati maana halisi ya nidhamu ambayo naijua mimi kwa umri wangu, labda haya ndiyo maendeleo ambayo mimi siyajui.

Suala la nidhamu ni la wazazi na kwa kiasi kikubwa linajengwa na kuendelezwa na walimu, lakini swali la msingi la kujiuliza;  ni kwa kiwango gani wazazi wanashirikiana na walimu katika kutatua mmomonyoko wa maadili ya watoto wetu? Wazazi wanashirikiana kwa kiwango gani katika kukabiliana na changamoto iliyopo katika makuzi ya wanetu?

Katika barua yangu ya wiki jana, nilisema kuwa sisi zamani kila aliyekuzidi umri alikuwa mzazi wako, na mwalimu yeyote wa shule yoyote alikuwa mwalimu wako. Hivi leo tunapaswa kujiuliza swali hili: Hivi ni kweli kwamba haya bado yapo ama yamepotea kutokana na maendeleo? Nasikia siku hizi huwezi kumwadhibu mtoto wa jirani yako hata kwa maneno, ni kesi kubwa.

Serikali kwa upande wake imechukua hatua gani katika kukabiliana na mwingiliano wa tabia za kimagharibi ili kulinda utamamduni wetu na kujenga taifa lenye heshima? Ni sahihi kwa viongozi kuacha kumbi za vileo ziwe huria, madanguro, picha chafu kwa watoto katika ‘vibanda umiza’, kuruhusu sherehe za vijana wa rika tofauti ufukweni, kuvuta bangi, kutumia dawa za kulevya, wizi uliokithiri kwa vijana, kuvaa nusu uchi, kutukana matusi ovyo na kadhalika?

Inawezekana lisiwe suala la serikali bali la wazazi, lakini mchango wa serikali katika kutoa msaada wa kisheria uko wapi? Leo hii tunasikia walimu wanapigwa na wanafunzi, wanaibiwa na wanafunzi, wanafanya ngono na wanafunzi, wanafunzi wanawazidi kipato walimu lakini kibaya zaidi ni kwamba wamevuka mipaka na kuhamia kwa wazazi wao kuonesha kuwa sasa hawana nidhamu kabisa!

Inaniwia vigumu kuamini kuwa tunaweza kushirikiana katika kutatua matatizo yaliyopo kwa kuwa mafiga matatu ya malezi hayakai na kutenga chungu. Serikali kwa upande mmoja, wazazi na jamii. Matokeo ya kuparaganyika kwa maadili ni mengi ikiwa ni kuwa na taifa lisilo na utamaduni wake, kupoteza amani iliyokuwapo na kukosekana kwa mwitikio mzuri wa elimu na matokeo yake ndiyo haya ambayo tumeanza kuyaona katika taifa letu.

Tunashuhudia upotevu wa amani, maandamano ambayo tunafikiri ya kidini, siasa, au mrengo mpya, kumbe ni taifa la vijana wenye maisha ya kufikirika, maisha ya tamaa na haraka ya mafanikio, maisha ya kugoogle kila kitu badala ya kutafuta kwa jasho na kupindishwa kwa sheria ambako sote mafiga matatu tunashirikiana kikamilifu.

Nauona umiliki wa nidhamu wa zamani kwa mafiga hayo matatu kwamba ndiyo yaliyotufundisha kusoma, kuheshimu, ukweli, kujali wengine, uzalendo, kujitegemea na upendo miongoni mwetu. Sitaki kuaminishwa kuwa sasa hivi hatuwezi kuyafanya hayo hadi tuone madhara makubwa zaidi. Vijana wanafunzi wawapende wazazi wao, walimu wao, viongozi wao.

Tugeuze fiesta kuwa picnic yetu, disko kuwa kuimba kwetu, camp kuwa chama chetu na kila mtu mkubwa kiumri kuwa mzazi wangu. Haya yatawezekana kama sote tutashirikiana kila mtu kwa nafasi yake.

 

Wasaalamu,

Mzee Zuzu,

Kipatimo.