ZANZIBAR VIJANA WAHAMASISHWA KUOA WAJANE

Mke wa Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Asha Suleiman Iddi amesema wajane wengi wanaweza kuondokana na changamoto zinazowakabili iwapo vijana wataamua kuwaoa.

Iddi alisema hayo katika utoaji wa zawadi kwa wanafunzi waliofanya vizuri katika mashindano ya kaswida yaliyoshirikisha madrasa 13 za Mkoa wa Mjini Magharibi.

Alisema wakati umefika kwa wanaume kuona umuhimu wa kuoa kutokana na kuongezeka matukio ya ubakaji ambayo yanaitia aibu nchi.

Iddi alisema jambo baya zaidi ni kuwa vitendo hivyo sasa vimehamia katika maeneo ya kusimamia masuala ya dini yakiwamo madrasa na misikitini, jambo ambalo linaifanya jamii kukosa amani katika maeneo yao.
Alisema inasikitisha kuona hali hiyo ya ubakaji ikitokea kwa watoto wenye umri mdogo, wakati kukiwa na kundi kubwa la watu wenye kuhitaji waume wakiwamo wajane.
#mwananchi