Rais wa Marekani Donald Trump amesema mazungumzo yake na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu hayakufikia hitimisho lolote la mwisho kuhusu Iran.
Trump amesisitiza kuwa mazungumzo na Tehran yataendelea akionyesha uwezekano wa kufikiwa kwa makubaliano mapya ya kidiplomasia.
Netanyahu, licha ya jitihada zake za kushinikiza msimamo mkali zaidi dhidi ya Iran, hakuonekana kupata ahadi alizokuwa akizitafuta kutoka kwa Trump.
Katika mkutano wao wa saba tangu Trump aliporejea madarakani mwaka jana, Netanyahu ambaye ziara yake ilikuwa ya kimya kimya kuliko kawaida, aliingia katika mkutano huo akiwa na lengo la kuishinikiza Marekani kupanua wigo wa majadiliano na Iran.
Netanyahu alitaka mazungumzo ya Washington na Tehran yasijikite tu kwenye mpango wa nyuklia bali pia yashughulikie mpango wa makombora ya masafa marefu wa Iran na kuzingatia uungaji mkono wa Tehran kwa makundi ya wanamgambo kama Hamas na Hezbollah.
Viongozi hao wawili walizungumza kwa faragha kwa zaidi ya saa mbili na nusu katika kile Trump alichokitaja kuwa “mkutano mzuri sana,” ingawa alikiri kuwa hakuna maamuzi makubwa yaliyofikiwa.



