Umoja wa Mataifa umeitolea wito Urusi kuacha kushambulia miundombinu ya nishati ya Ukraine, ambayo yamesababisha kukatika kwa umeme katikati ya kipindi cha baridi kali.

Mkuu wa Shirika la Haki za Binaadamu la umoja huo Volker Turk amesema mashambulizi yasiyokoma yanayofanywa na Urusi kwenye miundombinu kote nchini Ukraine yanawakosesha joto, maji na umeme raia ambao tayari wameteseka kwa muda mrefu.

Mkuu huyo wa haki za binaadamu amesema ni kinyume cha sheria ya kimataifa ya kiutu kuilenga miundombinu ya raia na kuitaka Urusi kusitisha mara moja mashambulizi hayo.

Ameongeza kuwa mamilioni ya makazi yanapitia kipindi kigumu kwa kuwa hupata umeme kwa masaa kadhaa ya siku, huku shule zisizo na vifaa vya joto zikilazimika kufungwa na huduma za tiba nazo zikiathiriwa.