Na Mwandishi Wetu, Zanzibar

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi Mhe. Hamza Hassan Juma amesema Serikali imeandaa mradi wa uvunaji wa maji ya mvua kwa kuweka mitaro ambayo yatawezesha maji kufuata mkondo wake na kuyajengea mabwawa ya kuzuia maji hayo.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya Habari Maelezo kuhusu siku 100 za mafanikio ya uongozi wa awamu ya pili ya Dkt. Mwinyi amesema tahmini hiyo tayari imewasilishwa Serikalini na kukabidhiwa Mamlaka husika kwa ajili ya utekelezaji.

Amesema jumla yya maeneo 30 yenye changamoto ya kutuama kwa maji ya mvua yamebainishwa na kutarajiwa kufanyiwa kazi ili kuondosha usumbufu kwa wananchi kuhama katika maeneo yao katika kipindi cha mvua.

Aidha Mhe. Hamza amesema Serikali imefanya tathmini juu ya changamoto za utiririshaji wa maji ya mvua ndani ya Mkoa wa Mjini Magharibi ili kutafuta suluhisho la kutuama kwa maji na kusababisha mafuriko katika maeneo mbali mbali.

Akizungumzia kuhusu eneo la Ziwa Maboga, Waziri Hamza ameeleza kuwa Serikali inatarajia kujenga bwawa la kisasa ili kuondosha usumbufu wa kutuama maji katika eneo hilo ambapo jumla ya nyumba 421 zimefanyiwa tathmini ili kupisha na ujenzi huo unatarajiwa kuanza mara baada ya wananchi kupewa fidia zao.

“Nawasisitiza wananchi kutoharibu miundombinu ya mitaro iliyowekwa na Serikali kwa kutupa taka katika mitaro ya kupitishia maji taka ili kuepuka athari katika kipindi cha mvua”

Waziri Hamza amesema kuwa Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais inaendelea kusimamia utaratibu wa shughuli za Mfuko wa maendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF) kwa upande wa Zanzibar kupitia mpango wa kunusuru kaya Masikini ambao unaendelea na hatua za matayarisho ya utekelezaji kwa awamu ya tatu.

“Zoezi la utambuzi wa kaya masikini lilifanyika kwa Shehia 75 za Unguja na Pemba ambapo jumla ya Kaya 14,818 zilitambuliwa na kuingizwa katika masjala ya walengwa wa Mpango wa TASAF” amefahamisha.